Mramba amsukumia zigo Balali

Waziri wa Fedha wa zamani, Basil Mramba

Waziri wa Fedha wa zamani, Basil Mramba (74), amedai mahakamani kuwa alimwelekeza aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Marehemu Daudi Balali, asisaini mkataba wa kuipa kazi kampuni tanzu ya Alex Stewart ( ASSAYERS) Government Business Corporation hadi atapofanya mazungumzo na Rais (wakati huo Benjamin Mkapa).

Mramba alitoa madai hayo jana wakati akihojiwa na wakili wa Serikali, Shadrack Kimaro, mbele ya jopo la mahakimu watatu wakiongozwa na Mwenyekiti  John Utamwa, Sam Rumanyika na Saul Kinemela wanaosikiliza kesi hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam.

Mshitakiwa huyo na wenzake wawili wanakabiliwa na mashtaka ya matumizi mabaya ya madaraka,  kutoa msamaha wa kodi kwa Kampuni ya Alex Stewart (ASSAYERS) ya Uingereza kupitia kampuni tanzu ya Alex Stewart (ASSAYERS) Government Business Corporation. 

“Nilimweleza Balali aanishe kwa sababu bado nilikuwa sijamaliza kazi kwa kumshauri Rais hatua za kukubali mkataba na kujua jinsi ya kupata fedha za mkataba huo kwa kuwa bajeti ya mwaka wa fedha ilikuwa imeshapitishwa (wakati huo),” alidai Mramba na kuongeza:

“Mkataba ule ulikuwa wa Serikali na ulilipwa kwa fedha za serikali, kwa sababu nilikuwa nimefunga bajeti ya mwaka huo, nilitaka kukutana na Rais kumshauri na kumuelekeza jinsi ya kupata fedha.”  Alidai kuwa maagizo yake kwa Gavana ya kufanya ainisho yalikuwa kujenga imani kwa mkandarasi kwa serikali kwamba ina nia ya kujenga na hatimaye itasaini mkataba huo.  Hata hivyo, kuhusu maelezo aliyohojiwa na kuyatoa kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuinisha mkataba, alidai kuwa alikuwa na maana ya kuinisho ni kuingia mkataba. 

Alidai kuwa, hajawahi kusomea mambo ya kodi bali alikuwa na mamlaka ya kusamehe kodi, kwamba alikuwa anapata ushauri kutoka kwa wataalamu wa masuala ya kodi kutoka Wizara ya Fedha na washauri wa jopo la wataalamu wa uchumi ambalo liliundwa kwa ajili ya kumshauri Waziri wa Fedha.

 Alidai, alikuwa anatumia vigezo vya kusamehe kodi kutokana na faida ya umma inayoweza kupata kama vile makampuni ya kutengeneza barabara na kwamba kukiwa na kodi kubwa makampuni yanaweza kukataa kutengeneza.  Mbali na Mramba washtakiwa wengine ni aliyekuwa Waziri wa Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu wa Hazina, Gray Mgonja

Katika kesi ya msingi, washitakiwa wanadaiwa kuwa, kati ya Agosti mwaka 2002 na Juni 14 mwaka 2004 jijini Dar es Salaam, wakiwa watumishi wa umma kama mawaziri na katibu mkuu walitumia vibaya madaraka.

 

JESHI la Polisi Mkoa wa Mbeya, linawashikilia watu 13, wakiwemo askari wawili wa Jeshi la wananchi (JWTZ) na polisi mmoja kwa matukio ya mauaji na unyang'anyi wa kutumia silaha.

Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya  Diwani Athuman akiwa na viongozi wenzake wa jeshi hilo la polisi wakati wa kuongea na waandishi wa habari wa Mbeya
Siraha zilizokamatwa na na jeshi hilo la polisi ndizo zilikokuwa zinatumika na majambazi hayo 
Moja ya bastora iliyotengenezwa kienyeji kwa kutumia vipande vya bomba lakini inatumia risasi za kawaida na nihatari sana siraha hii
Hizi ni vifaa vilivyokamatwa katika matukio mbalimbali yaliotokea mkoani hapa kamanda amewaomba wananchi wa mbeya kuja kuvitambua ofisini kwakwe 
Hizi ni siraha na sare za jeshi ambazo walikuwa wanatumia majambazi hao waliokamatwa kwa tuhuma za mauaji
Waandishi wa habari wakimsikiliza kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya
Mfanyabiashara maarufu wa eneo la Mwanjelwa, Gath Mbilinyi (32), anaetuhumiwa kuteka na kuua
Hawa ndiyo wanaotuhumiwa  kuwaua  dereva na utingo wake na kisha kwenda kuwazika porini  
Samahani kwa picha hizi zinasikitisha haya niamabaki ya miili ya tingo na dereva wake waliouwawa na watuhumiwa hapo juu


JESHI la Polisi Mkoa wa Mbeya, linawashikilia watu 13, wakiwemo askari wawili wa Jeshi la wananchi (JWTZ) na polisi mmoja  kwa matukio ya mauaji na unyang'anyi wa kutumia silaha.

Akizungumza na waandishi habari jijini Mbeya Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya  Diwani Athuman amesema watuhumiwa hao wamewagawanya katika makundi mawili, ambapo kundi la kwanza ni la watuhumiwa 9 wakiwemo askari hao wawili wakidaiwa kuhusika na tukio la kuwaua kikatili na kisha kuwazika dereva na utingo wake.

kundi la pili ni la watuhumiwa wanne wanaotuhumiwa kuhusika na mauaji ya dereva wa polisi lililotokea Wilayani Chunya mkoani hapa baada ya kufanyika uporaji wa shilingi milioni 2,200,000 katika kituo cha mafuta eneo la Matundasi wilayani chunya.

Akitoa ufafanuzi zaidi Kamanda Diwani amesema, katika tukio la kwanza ni lile lililotokea Februari 2 katika eneo la Mafinga,Mkoani Mbeya, ambapo watuhumiwa wa kundi la kwanza waliwateka dereva na utingo wake, Festo Kyando (45) na Jafari lililotokea na kuwaua kisha kwenda kuwazika porini.

Amesema dereva huyo alikuwa ametoka Jijini Dar es salaam kubeba mzigo wa wafanyabiashara kwa lengo la kuleta mkoani Mbeya, lakini kumbe walikuwa wakiwindwa na walipofika mkoani Iringa walitekwa na kufanyiwa mauaji hayo ya kinyama.

Kamanda Diwani amesema kufuatia tukio hilo jeshi la polisi lilianza uchunguzi mkali na hatimaye kunasa mtandao huo wa watu 9 wakiwemo askari hao wawili wa jeshi la polisi na JWTZ,ambao uchunguzi umebaini kuwa hutoa mavazi ya majeshi hayo na silaha.

Kamanda Diwani amewataja watuhumiwa hao kuwa MT.85393 Samwel Charles  Balumwina(31) wajiriwa wa jeshi la wananchi kikosi 844 kikosi cha Itende Mbeya na G.1901PC Samwel Kigunye (27) askari wa jeshi la polisi Jijini Mbeya.

Wengine ni mfanyabiashara maarufu wa eneo la Mwanjelwa, Gath Mbilinyi (32), Rajabu Mbilinyi(25), Gregory Mtega(25,Francis Sanga(30) pamoja na ndugu ambao ni wafanyabiashara maarufu katika mji wa Makambako mkoani Njombe ambao ni Japhet Ng'ang'ana(24), Claud Ng'ang'ana(36), Hilally Ng'ang'ana(30)

Hata hivyo amesema walifanikiwa kukamata bidhaa hizo katika eneo la Tunduma ambako tayari zilikuwa zimekamatwa na kwamba miongoni mwa watuhumiwa ndiye aliyeuziwa mzigo huo.

Amesema mali zilizookolewa katika matukio hayo kuwa ni Nondo 397 za aina tofauti pamoja na bando 18 za mifuko ya sandarusi(Sulphate) ambavyo vinashikiliwa na jeshi la Polisi Tunduma Wilani Mbozi Mkoani hapa.

Katika tukio la pili ni lile linalohusisha vifo vya watu wawili wilayani Chunya, ambao ni dereva wa polisi na dereva wa gari la majambazi baada ya kutokea kurushiana risasi.
Amesema tukio hilo lilitokea Februari 6 baada ya watuhumiwa wanne ambao wanashikiliwa na jeshi hilo kufanya uporaji wa shilingi milioni 2,200,000 katika kituo cha matundasi wilayani humo.
Amewataja madereva hao waliouwawa katika tukio hilo kuwa ni dereva wa polisi aliyefahamika kwa jina moja la Jafari, ambapo yule wa majambazi akitajwa kwa jina la  Shabani John.
Diwani amewataja watuhumiwa wanashikiliwa kwa tukio hilo kuwa ni Manase Kibona (37).Emmanuel Mndendemi na Masai Hongole, Mashaka George, John Mahenge, Narasco Mabiki.

Kamanda huyo amezitaja mali zilizookolewa katika matukio hayo kuwa ni Nondo 397 za aina tofauti pamoja na bando 18 za mifuko ya sandarusi(Sulphate) ambavyo vinashikiliwa na jeshi la Polisi Tunduma Wilani Momba  Mkoani Mbeya.

Aidha,kamanda Diwani  amevitaja baadhi ya vielelezo vilivyokamatwa  kuwa ni Bunduki aina ya Shot Gun moja ambayo namba zake zilifutika, Gobore moja ambalo pia namba zake zilifutika, Bastora tatu zilizotengenezwa kienyeji zisizo na namba na zinazotumia risasi za s/Gun.

Vingine ni Risasi 31 za Silaha ya SMG/SAR, Sare za Jeshi (JWTZ), suruali 4, mashati 4 kofia 3 na Viatu jozi mbili , Risasi 99 za S/GUN, Risasi 25 za Bastola na magari yenye namba T 464BLX TOYOTA COROLA,T381 BDR VITZ, T 251 AKU Toyota Pick Up ,T 193 BDY  Toyota Premio na T 214 ASV  Toyot Mark II.

Hata hivyo Kamanda wa Polisi anawashukuru wananchi wa Mkoa wa Mbeya waliojitokeza katika ktoa ushirikiano wa kuwasaka majambazi hayo ambapo pia anaendelea kutoa wito kwa watu wenye taarifa za watu ambao haeajakamatwa.
Ameongeza kuwa taratibu za upelelezi zimekamilika ambapo taratibu za kuwafikisha mahamakamani zinaendelea.

Polisi watumia nguvu kuzuia maiti kusafirishwa Geita

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Leonard Paulo 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Leonard Paulo alikuwapo wakati askari wake walipoingilia msafara huo na kusababisha vurumai kubwa.
Waombolezaji hao walikuwa wakiuhamisha mwili wa marehemu Fungungu kutoka Hospitali ya Runzewa kuupeleka katika Hospitali ya Geita.


Sakata hilo la ndugu na polisi lililotokea saa nane mchana juzi Jumamosi katika Pori la Samina, Geita na polisi wakiwa kwenye magari matatu wakiwa wamesheheni silaha mbalimbali walifika na kuzuia mwili wa marehemu kusafirishwa.


Baadhi ya ndugu wa marehemu akiwamo mkewe, wanadai kwamba Fungungu alifariki dunia baada ya kupigwa risasi na polisi wanaosemekana kwamba walimvamia nyumbani kwake usiku wa kuamkia Alhamisi iliyopita kisha kupora mamilioni ya fedha. Wanadai kwamba alipigwa risasi tumboni na kichwani katika Kijiji cha Runzewe, Wilaya ya Bukombe mkoani hapa.


Katika tukio hilo inadaiwa kuwa kiasi cha Sh360 milioni kiliporwa. Kati ya fedha hizo, Sh60 milioni zinadaiwa kwamba zilikuwa kwenye gari wakati Sh300 milioni zilikuwa kwenye masanduku mawili yaliyokuwa ndani ya nyumba.


Pia ndugu hao walidai kwamba Sh1.2 milioni zilichukuliwa na askari wawili wa kiume baada ya kumpekua mke wa marehemu kwenye nguo za ndani.


Pia askari hao wanadaiwa kupora mali mbalimbali za marehemu zikiwamo redio mbili, video kamera moja, nguo za marehemu ikiwamo kanzu, mashine ya printer, mashine ya inventor, karatasi za picha, deki mbili za kucheza CD, pamoja na nguo za mke wa marehemu.


Mapema Kamanda Paulo alikuwa ameeleza kuwa marehemu alijiua mwenyewe baada ya kumjeruhi Polisi, Fortunatus Beatus kwa risasi lakini taarifa hizo zimepingwa vikali na ndugu na jamaa wa marehemu ambao wanadai marehemu aliuawa na polisi akiwa nyumbani kwake.

Polisi kuzuia waombolezaji

Baada ya polisi kuyasimamisha magari manane yaliyokuwa katika msafara huo wa kupeleka mwili wa marehemu kwenda kuhifadhiwa katika chumba cha maiti Hospitali ya Geita, kulizuka mabishano makali kati ya Kamanda Paulo na ndugu wa marehemu.


Inadaiwa kwamba polisi walikuwa wakishinikiza mwili huo urejeshwe Runzewe, Bukombe kwa kuwa tayari ulikuwa umefanyiwa uchunguzi jambo ambalo liliwakera waombolezaji hao.


Kabla ya kamanda huyo kufika eneo hilo, msafara huo ulisimamishwa na Polisi wa Usalama Barabarani ambao walikuwa wamefuatana na wale wa Kutuliza Ghasia (FFU), wakiongozwa na Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Geita, Leonard Makona.
Baada ya kuusimamisha msafara huo, Makona aliwataka ndugu wa marehemu kumsubiri Kamanda Paulo ambaye alifika baada ya takriban dakika 10.


Mwandishi wa habari hii ambaye alikuwa katika eneo la tukio, alishuhudia ndugu wa marehemu na Kamanda Paulo wakirushiana maneno.


“Mnapeleka wapi mwili wa marehemu, ina maana hamkuridhika na uchunguzi wa daktari wa Bukombe?” alihoji kwa ukali na kujibiwa pia kwa ukali na kaka wa marehemu, Mariatabu Fungungu: “Kwa nini mnatusimamisha? Tunaomba tuite waandishi wa habari hapa ili waje washuhudie tukio hili. Kwa nini msikae ofisini?”

 Baadaye, kamanda huyo aliwaamuru askari wake kuwaingiza katika gari la polisi ndugu watano wa marehemu wakiwamo mke wa marehemu, Lucia Kilaza (23) na Mariatabu. Walifanya hivyo kwa kutumia nguvu na kisha kuondoka nao hadi katika Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Geita.


Ndugu wa marehemu walilalamikia kitendo hicho wakisema kilikuwa na lengo la kuficha ukweli wa tukio hilo.

Mke wa marehemu

Kilaza alidai kuwa kifo cha mumewe kilitokea baada ya zaidi askari 20 kuvamia nyumbani kwake yapata saa tisa usiku na kumwamuru Fungungu kutoka nje na alipogoma, ndipo walipoanza kupiga risasi na kuvunja vioo vya madirisha na milango na risasi kumpata marehemu. Pia alidai kuwa walipiga mabomu ya machozi.


Alisema baada ya tukio hilo, walivunja mlango na kuingia ndani kisha kumchukua mumewe ambaye tayari alikuwa amefariki na kumtupa nje... “Mimi pia walinichukua wakanitupa nje ya uzio baadaye wakaanza kunipekua nguo za ndani na kuchukua Sh1.2 milioni ambazo nilikuwa nimezificha baada ya kuona wameanza kufyatua risasi.”


Wakizungumzia tukio hilo, Mbunge wa Bukombe, Profesa Kalikoyela Kahigi na Diwani wa Runzewe, Yusufu Fungameza walisema Serikali inatakiwa kuingilia kati suala hilo ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua za kisheria waliohusika katika tukio.


Alipotakiwa kuzungumzia tukio hilo, Kamanda Paulo aliwaahidi waandishi wa habari kwamba angelitolea ufafanuzi jana Jumatatu. Hata hivyo, alishindwa kufanya hivyo kwa madai kwamba anapisha kwanza uchunguzi wa mwili wa marehemu kwenye Hospitali ya Geita.


Ndugu wa marehemu wamegoma kuuzika mwili wa marehemu wakitaka uchunguzi wa kina ufanyike kwa kutumia jopo maalumu la madaktari huku wakiitaka Serikali kuunda tume kuchunguza tukio hilo.

Mtandao wa ujambazi Mbeya

Katika hatua nyingine; Watu wanaodaiwa kujihusisha na matukio ya uhalifu katika mikoa ya Mbeya, Iringa, Morogoro na Dar es Salaam wamenaswa na polisi huko Mbeya.
Mtandao huo unadaiwa kuwahusisha askari mmoja wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) pamoja na wafanyabiashara maarufu wa Mbeya.


Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Diwani Athumani alisema jana kuwa watu 29 wanaodaiwa kujihusisha na mtandao huo wanashikiliwa na jeshi hilo.


“Askari hao mbali na kujihusisha na matukio ya ujambazi moja kwa moja, pia walikuwa na tabia ya kuwaazima majambazi sare za jeshi ambazo zilikuwa zikitumika kwenye matukio mbalimbali ya uhalifu,” alisema.


Alisema watuhumiwa wote hao wanakabiliwa na tuhuma za mauaji, ujambazi na kupokea mali za wizi na walikamatwa katika maeneo ya Mkwajuni, Chunya na Makambako na Mafinga, Iringa.


Kamanda Athumani alisema kuwa watuhumiwa 13 watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma za ujambazi, mauaji na kupokea mali za wizi, wengine saba watasafirishwa kwenda Iringa ambako ndiko watakakofikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.


Kamanda Athumani alisema uchunguzi wa watuhumiwa wengine 16 bado unaendelea na wataachiwa kwa dhamana na watatakiwa kuripoti vituo vya polisi watakavyopangiwa.

viziwi wa mji mdogo wa kibaingwa washindwa kuchangia marekebisho ya katiba


Na John Banda,Dodoma

VIZIWI wanaoishi vijijini wa mji mdogo wa Kibaingwa Wilaya ya Kongwa wale wanaoishi vijijini ,wamesema watashindwa kuchangia mawazo yao ya marekebisho ya katiba mpya inayoendelea kwa hivi sasa kwa kuwa hawajawahi kukiona kitabu cha katiba na pia hawajawahi kukisoma bali wanasikia kupitia kwenye vyombo vya habari ikitanganzwa.

Kauli hiyo imetolewa kwa pamoja na walemavu Tito Mnyamale (33) na Paul Mnage (32) kwa niaba ya wezao wakati wanapokuwa wakichangia juu ya marekebisho yanayotakiwa yafanyike kuhusu haki zinazotakiwa kutendewa watu wenye ulemavu wa kutosikia.

Wakichangia hoja zao kwenye warsha ya mafunzo ya mkataba wa umoja wa mataifa juu ya haki ya walemavu na sheria na sera ya Taifa ya viziwi mwaka 2010 kwa viziwi wa mji wa mamlaka ya Kibaingwa Wilaya ya Kongwa.

Walemavu hao walisema wanashindwa kuchangia katiba hiyo kutokana na kutoielewa na itawasaidiaje wao wakati toka wamezaliwa hawajawahi kuiona na badala yake wanaisikia kwenye vyombo mbalimbali vya habari.

"Hapa lazima tuiambie ukweli serikali yetu kuwa sisi walemavu tunaoishi vijijini hatujakiona hiki kitabu ambacho leo hii tunaambiwa ndiyo katiba inayotakiwa kufanyiwa marekebisho mbalimbali,hii pia inatokana na kwa upande wetu kukosa kushirikishwa kwenye vikao vinavyozungumzia marekebisho hayo ya katiba"alisema Mnange.

Aidha walemavu hao walisema kutokana na viongozi wa serikali ngazi ya kata,vijiji hadi vitongoji kitendo chao cha kutowashirikisha kwenye vikao vya kujadili katiba hiyo pia kumechangia kwa upande wao kutoipata elimu ya kutosha ambayo ingetuwezesha kufahamu namna ya kuijadiri marekebisho hayo.

"Serikali yetu kwa kupitia viongozi wao wamekuwa wakiwaona wa maana sana katika kipindi cha upigaji kura tu,na wako radhi kuja kutubeba kwa usafiri wao ili waweze kupigiwa kura za kuwachangua lakini kwenye suala la kujadili mapendekezo ya marekebisho ya katiba inaonekana sisi haituhusu kabisa"alisema Tito.

Naye Meneja wa mradi wa Leonard Cheshine Disibility Dodoma Baraka Mgohamwende aliwataka walemavu hao kutoa maoni yao juu ya haki wanazotaka zifanyiwe kwa kupitia katiba hiyo mpya ambayo hivi sasa inajadiliwa na kupendekezwa na watanzania hapa nchini.

Mgohamwendo ambaye alikuwa akielimisha umuhimu wa kuitambua katiba kwenye warsha hiyo, alisema kuwa pamoja na kutoielewa maana ya katiba hiyo ambayo hivi sasa wameiona na kukabidhiwa,wanatakiwa kuisoma ili kupitisha maoni yao ambayo yanayohitajika kuwepo na haki zao zinazotakiwa waweze kufanikisha.

Naye Katibu wa Chavita wilaya ya Kongwa Anitha Masawe alisema katika eneo hilo walemavu wa Uziwi walio wengi hawaitambui katiba hiyo inatokana viongozi walio kwenye ngazi za vitongoji,vijiji na kata kwa upande wa serikali na siasa hawaoni umuhimu wa kuwashirikisha shughuli mbalimbali za kimaendeleo.

Anitha alisema ndiyo maana leo hii walemavu wa wilaya hiyo hususan wale wanaoishi vijijini,hawajui katiba na faida ambazo watakazoziona kama na wao watachangia katika kutoa mapendekezo ya marekebisho ya katiba hiyo.

Mwisho.

JICHO LETU KATIKA MAGAZETI FEB.25

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.