Maduka yafungwa Dodoma wenyewe wagomea mashine za kieletroniki EFDs za TRA


  
  
 
 Maduka yakiwa yamefungwa katika mitaa mbalimbali ya manispaa ya Dodoma baada ya wafanyabiashara kugoma kuazia jana karibu nchi nzima kwa muda usiyojulikana huku mapendekezo yao kuwa gharama za uendeshaji mashine hizo zifanywe na serekali.
 
 Baadhi ya wafanyabiashara wa maduka wakipiga soga nje ya maduka yao baada ya kuyafunga kwa muda usiyojulikana wakipinga mashine ya kielektroniki EFDs iliyotolewa na TRA na kutakiwa kila mfanyabiashara kuwa nayo.
[PICHA NA JOHN BANDA]

Wajitokeza na kudai watoto wa Mandela


Pretoria. Wanawake wawili wanaodai kuwa watoto wa Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, wamejitokeza na kutaka watambuliwe kwenye mirathi ya familia yake.

Kwa mujibu wa mwanasheria anayesimamia mirathi hiyo, Michael Katz, wanawake hao wanadai kwamba ni watoto wa Mandela na kwamba wanashangaa kutotajwa katika mirathi yake iliyotangazwa wiki iliyopita.

Wakili Katz alisema wawakilishi wa wanawake hao, Onica Mothoa na Mpho Pule, wamewasiliana naye wakitaka utata uliopo sasa utatuliwe, ili nao waweze kupata haki yao kama watoto wengine wa marehemu.

Katz alisema, Mothoa na Pule wanadaiwa kuzaliwa na Mandela wakati akiwa katika ndoa ya mke wake wa kwanza, Evelyn Mase, aliyeachana naye mwishoni mwa miaka ya 1950.

Taarifa ya kipindi cha televisheni cha Carte Blanche, iliripoti juzi jioni kwamba tayari wanasheria wawili wanaowawakilisha wanawake hao, wameshawasiliana na wasimamizi wa mahakama, kutaka kusitishwa mgawanyo wa mali kama ilivyoelezwa katika wosia wa mirathi wa Mandela, hadi suala hilo litakapopatiwa ufumbuzi.

Naibu Jaji Mkuu, Dikgang Moseneke, aliwaeleza wanahabari Jumatatu wiki iliyopita kwamba mali za Mandela zinafikia Randi 46 milioni (sawa na Sh5.6 bilioni).

“Kiasi hicho hakijumuishi mapato yatokanayo na kazi zake nyingine na uwekezaji aliowahi kuufanya,” alieleza.

Wosia wa mgawanyo wa mali zake uliandikwa mwaka 2004 na kurekebishwa kwa mara ya mwisho mwaka 2008.

Mwanasheria Katz, alisema wanawake hao wanataka kutambuliwa rasmi katika wosia wake na si kwamba wanahitaji kiasi chochote cha fedha.

Alisema anatarajia kukutana na wasimamizi wa wosia wa Mandela kwa ajili ya kujadili kwa kina kuhusu suala hilo.

Katika kipindi cha Carte Blanche, watu wa karibu wa Mothoa na Pule walidai kwamba waliwahi kujaribu kuzungumza na Mandela ili akubali kwamba ni baba halisi wa watoto hao.

Hata hivyo, hakuwahi kujibu au kutoa msimamo wake.

 

Ukumbi bunge la Katiba sasa wakamilika





Spika wa Bunge, Anne Makinda (aliyekaa) akiwa na Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Bunge wakati wakikagua Ukumbi wa Bunge, ambao utatumika kwa ajili ya Bunge la Katiba, mjini Dodoma jana. Picha na Ofisi ya Bunge 


Dodoma. Matengenezo yaliyotarajiwa ndani ya ukumbi wa bunge la Muungano ambao ndio utakaotumika kwa bunge la Katiba, yamekamilika na sasa ukumbi huo uko tayari kwa kazi inayotarajia kuanza Februari 18 mwaka huu.

Kukamilika kwa ukumbi huo kunaondoa hofu iliyoanza kutanda kuwa huenda bunge hilo lingesogezwa mbele kwa siku tatu kwani kulikuwa na mashaka kwa kazi hiyo.

Jana Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi alitembelea ukumbi huo kwa mara ya mwisho na kujiridhisha katika maeneo muhimu yaliyokuwa yakifanyiwa marekebisho .

Akizungumza na waandishi wa habari ndani ya ukumbi huo, Lukuvi alisema tayari viti 676 vimeshafungwa pamoja vipaza sauti vyake ambavyo Rais Jakaya Kikwete alionyesha mashaka kama vingekamilika kwa wakati.

Februari Mosi, Rais Kikwete alipita kukagua ukumbi huo wakati akielekea mkoani Mbeya ambapo alionyesha kutokuridhika hasa akatilia mashaka katika eneo la vipaza sauti ambako alisema kuwa bado kulikuwa na kazi kubwa ya kufanya.

Hata hivyo, jana Lukuvi licha ya kushuhudia kuwa vimefungwa katika viti vyote, lakini alipotakiwa na waandishi kuwasha kwa majaribio, wajenzi wa ukumbi walizuia na kusema kitaalamu hakutakiwa kuwasha jana kwani kazi ilikuwa bado inaendelea.

Alisema kuwa Ofisi ya Bunge imeshatafuta kumbi nyingine nje ya bunge kwa ajili ya kufanyika mikutano ambayo itahitaji wajumbe zaidi ya 60.

Mgomo kila kona kuzipinga EFDs


Mikoani. Sakata la matumizi ya Mashine za Elektroniki za Kutolea Risiti (EFD), limechukua sura mpya baada ya wafanyabiashara mikoa mbalimbali kuja juu wakisema matumizi yake yanalenga kuwaangamiza katika biashara.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wafanyabiashara hao wameitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kufikiria upya mfumo wa kuzitumia, vinginenyo watajikuta wanaingia kwenye mgogoro mkubwa baina yao.

Tayari, wafanyabiashara miji ya Iringa, Songea na Mara wametoa msimamo wa kugomea matumizi ya mashine hizo na kuazimia kufunga biashara zao kama njia ya kupinga matumizi yake.

Wafanyabiashara wa Manispaa ya Iringa, jana walitangaza mgomo usio na kikomo kwa sababu mashine hizo zinawasababishia hasara. Wanadai mashine hizo licha ya kununuliwa kwa bei kubwa, inawabidi kuajiri wafanyakazi wenye ujuzi na kodi nyingine wanajikuta wakitumia sehemu za mitaji yao.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk Christine Ishengoma aliwataka wafanyabiashara kuacha migomo isiokuwa na tija wala sababu, badala yake wafikishe malalamiko yao kwa uongozi husika kupitia viongozi wao.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara wa Viwanda na Kilimo (TCCIA) mkoani Mara, Baltazar Gibogo alisema mgomo huo ni halali yao, kwani Serikali inawanyanyasa wananchi wake.

Gibogo alikanusha kuwa Serikali imeshindwa kukusanya kodi hadi kubuni kutumia mashine, bali chanzo kikubwa ni kukithiri kwa rushwa baina ya wafanyabiashara wakubwa na wafanyakazi wa TRA.

Mjini Mbeya, wafanyabiashara walishauri Serikali kuzitoa bure mashine za EFD ili kuwasaidia wafanyabiashara kujijenga kibiashara badala ya kufilisika.

“Pamoja na kwamba Mamlaka ya Mapato tanzania (TRA) inasema mfanyabiashara akinunua anaweza kurudisha fedha zake kwa kupunguza zile za kodi, ukweli unabaki palepale kwamba wafanyabiashara hawana fedha taslimu kununua kitu ambacho siyo cha kuuza na kupata fedha kwa wakati huo,’’ alisema Anania Kasisi.

Imeandikwa na Florence Focas , Musoma; Geofrey Nyang’oro na Zainab Maeda, Iringa na Lauden Mwambona, Mbeya

Mwenyekiti wa CCM Dar kizimbani kwa tuhuma za kusambaza ARV feki

 
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Industries Limited (TPI), Ramadhani Madabida (kulia) na Ofisa Ubora wa Bidhaa wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD), Evance Mwemezi walipofikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam jana kusomewa mashtaka ya kuuza na kusambaza dawa feki za ARV. Picha na Venance Nestory 


Dar es Salaam. Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Tanzania Pharmaceutical Ltd cha Dar es Salaam (TPI), Ramadhani Madabida na wenzake watano wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka matano likiwamo la kusambaza dawa bandia na kusababisha hasara ya Sh148.3 milioni.

Wakili wa Serikali, Faraja Nchimbi aliwataja washtakiwa wengine wanaokabiliwa na kesi hiyo kuwa ni Mkurugenzi wa Operesheni wa TPI, Seif Shamte, Meneja Masoko, Simon Msofe, Mhasibu Msaidizi, Fatma Shango pamoja na wafanyakazi wa Bohari ya Dawa (MSD), Sadick Materu na Evans Mwemezi.

Akisoma hati ya mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Nyigulile Mwaseba, Wakili wa Serikali, Shadrack Kimaro alisema katika shtaka la kwanza, Aprili 5, 2011, Madabida, Shamte, Msofe na Shango wakiwa na nyadhifa hizo kwenye kiwanda cha TPI walisambaza makopo 7,776 ya dawa bandia za kufubaza virusi vya Ukimwi (ARV) aina ya Antirectroviral.

Kimaro alidai kuwa washtakiwa hao, walifanya kosa hilo kinyume na kifungu cha 76 (1)(2) cha Sheria ya Chakula, Dawa na Vipodozi ya mwaka 2003, wakijaribu kuonyesha kuwa dawa hizo zilikuwa halali na kwamba zimetengenezwa Machi, 2011 na muda wake wa kutumika unakwisha 2013 wakati wakijua kuwa si kweli.

Katika shtaka la pili, Wakili Kimaro alidai kuwa Aprili 11, 2011, Madabida, Shamte, Msofe na Shango walisambaza na kuuza makopo 4,476 ya dawa bandia aina ya Antiretroviral walizokuwa wakijaribu kuonyesha kuwa zilikuwa na viambatanisho vya Starudine 30mg, Nevirapine 200mg, Lamivudine 150mg pamoja na fungu namba OC 01.85.

Alidai kuwa washtakiwa hao waliweka viambatanisho hivyo wakijaribu kuonyesha kuwa dawa hizo zilikuwa halisi na kwamba zilitengenezwa Machi 2011 na muda wake wa kutumika ulikwisha Februari 2013 huku wakijua kwamba ni uongo.

Katika shtaka la tatu wanadaiwa kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu, kinyume na Kifungu cha 302 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Wakili Kimaro alidai kuwa kati ya Aprili 12 na 29, 2011, washtakiwa hao wakiwa na nia ya kulaghai, walijipatia Dola za Marekani 98,506 sawa na Sh148,350,156.48 wakijaribu kuonyesha kuwa kiasi hicho cha fedha ni malipo halali ya makopo 12,252 ya dawa aina ya Antirectrovial yaliyokuwa katika fungu (batch) namba OC 1.85.

Alidai pia kuwa washtakiwa hao walikuwa wakionyesha dawa hizo bandia zilikuwa zimetengenezwa Machi, 2011 na kwamba muda wake wa kumalizika kutumika ni Februari, 2013 na wakafanikiwa kujipatia kiasi hicho cha fedha kutoka MSD.

Katika shtaka la nne, Materu na Mwemezi wakiwa ni Meneja wa Udhibiti Viwango na Ofisa Udhibiti Viwango wa MSD, kati ya Aprili 2 na 13, 2011 huku wakijua nia ya kutendeka kwa makosa hayo ya usambazwaji wa dawa bandia, walishindwa kuzuia kinyume na Kifungu cha Sheria namba 383 cha Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Katika shtaka la tano, wakili huyo wa Serikali alidai kuwa kati ya Aprili 5 na 30, 2011, washtakiwa Madabida, Shamte, Msofe, Shango pamoja na Materu na Mwemezi, kinyume na Sheria ya Uhujumu Uchumi, walishindwa kutekeleza majukumu yao wakiwa watendaji.

Alidai kuwa katika kipindi hicho, washtakiwa hao kwa pamoja walishindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwa kusambaza makopo 12,252 ya dawa bandia wakijaribu kuonyesha kuwa zilitengenezwa Machi 2011 na kwamba zitakwisha muda wake wa kutumika Februari 2013 na kuisababishia mamlaka hiyo ya Serikali hasara ya Sh148,350,156.48.

Washtakiwa wote walikana mashtaka yanayowakabili na upande wa mashtaka ulisema upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika. Akitoa masharti ya dhamana, Hakimu Mwaseba alimtaka kila mshtakiwa kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika ambao wanafanya kazi kwenye taasisi zinazotambulika kisheria na kwamba kila mdhamini angesaini bondi ya Sh6,181, 256.

Pia alimtaka kila mshtakiwa kutoa kiasi cha Sh12, 362,513 milioni taslimu mahakamani hapo au hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya kiasi hicho cha fedha.

Madabida na Materu waliachiwa huru baada ya kukamilisha masharti hayo huku wenzao wakipelekwa mahabusu kusubiri kuyakamilisha.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Februari 24, mwaka huu itakapotajwa.