Ubakaji India : Aliyemtetea mbakaji kufutiwa leseni

Baadhi ya waandamanaji wakiandamana kupinga vitendo vya ubakaji.


Tofauti na Tanzania, nchini India Serikali inaonekana kuwawajibisha ipasavyo wenye kuendesha vitendo vichafu vikiwamo vya ubakaji.

Lilivyo kubwa tatizo la ubakaji nchini India, ni sawa na hapa kwetu Tanzania lilivyo la dawa za kulevya. Hata hivyo, tofauti kubwa ni namna viongozi wanavyotoa uamuzi kwa wenye kutenda maovu. Wiki hii nchi hiyo imetoa hukumu ambayo imetoa matumaini kwa wananchi wake.

Mfagizi,  Akshay Thakur, Mwalimu wa Mazoezi,  Vinay Sharma, Muuza Matunda, Pawan Gupta na Mukesh Singh walihukumiwa kifo baada ya kupatikana na hatia ya kubaka, kuua na kula njama za kupoteza ushahidi.

Mahakama iliwahukumu wote wanne kunyongwa na mmoja ambaye alikuwa chini ya umri wa miaka 18, mwezi uliopita alihukumiwa kifungo maalumu cha miaka mitatu.

Hata hivyo wakati hukumu hiyo ikiwa katika hatua za utekelezaji, wakili, AP Singh aliyekuwa akiwatetea watuhumiwa wawili kati ya hao huenda akafutiwa leseni yake.

Singh ameingia matatani baada ya kutoa kauli ambayo imewakera mawakili wenzake na kumwamuru aombe msamaha na iwapo hata fanya hivyo atafutiwa leseni yake.

Wakili huyo baada ya kusikia hukumu hiyo aliwaambia waandishi wa habari kuwa, mwenye makosa katika kesi hiyo ni binti huyo ambaye alikuwa akitembea usiku.

“Binti yangu akitembea usiku kama huyu, nitamnyonga mbele za watu, tunatakiwa tuwafundishe adabu mabinti zetu ili wasipate mabalaa kama haya, tukio hili liwe fundisho,” anasema Singh.

Umoja wa Wanasheria nchini India, The Delhi Bar Council (DBC) umemtaka Singh kuomba msamaha kwa jamii na familia ya binti huyo kwa kuwa kama mwanasheria alipaswa kusimamia haki.

Katibu wa umoja huo, Murari Tiwari amesema Singh anapaswa kuomba radhi kwani kitendo chake cha kukubali kuwatetea watuhumiwa wa ubakaji na kauli yake, vinashusha hadhi yake.

Hata hivyo Singh amesema anasimamia kauli yake na anajivunia kuwa mmoja wa watetezi wa vijana hao. Ameongeza kuwa anasubiri kufutiwa leseni naye atachukua hatua nyingine kupigania haki yake kama wakili.

Shambulio la kutisha

Binti wa miaka 22 akiwa na mpenzi wake walitekwa baada ya kupanda basi walilokuwemo wabakaji hao. Walikuwa wakitokea kuangalia sinema, wakalisimamisha basi hilo.

Mwanamume ambaye alinusurika katika tukio hilo anasema baada ya kuwateka waliwapiga , kuwang’ata kwa meno na kisha kuingiza chuma katika sehemu za siri za mwanamke huyo.

Baadaye waliwatupa kandokando ya barabara na wao kutokomea. Walipoamka walijikuta hospitalini lakini hali ya mwanamke ilikuwa mbaya zaidi na alihitaji matibabu ya hali ya juu. Alipelekwa nchini Indonesia hata hivyo hakupona  na kufariki dunia wiki mbili baadaye. Nchini India kuna zaidi ya kesi 1,098 za ubakaji.

Ingawa familia za watuhumiwa zinasema Serikali imewatumia vijana hao kama njia ya kuwaridhisha raia wake, lakini vipimo vya vinasaba (DNA) katika alama za meno zinaonyesha ni za vijana hao. Hata mwanamume aliyenusurika katika tukio hilo anathibitisha kuwa washambuliaji ni vijana hao sita.

“Binti yangu amepata haki leo, tumefurahishwa sana na hukumu hii,” anasema baba wa binti aliyefariki katika tukio hilo.

Wakati hukumu hiyo ikisomwa, baba wa binti huyo alikuwa amekaa chini  amejiinamia huku akibubujikwa machozi lakini ghafla aliibuka na kuruka juu baada ya kusikia wamehukumiwa kunyongwa.

Anasema tangu binti yake aliposhambuliwa, alibatizwa jina la Nirbhaya ambayo maana yake ni Isiyo na Woga.

Nirbhaya amekuwa nembo ya wanawake ambao hushambuliwa kila baada ya dakika 21. Nchini India matukio ya ubakaji, udhalilishaji na matukio ya kumwagiwa tindikali hutokea kila baada ya dakika 21.

Hukumu hiyo itapelekwa mahakama kuu ya nchi hiyo na majaji wawili wataiangalia na kuipitisha au kuifuta adhabu hiyo.Hata hivyo utekelezaji wake unaweza kuchukua miaka mingi.

Tangu kuanza kusikilizwa kwa kesi hiyo, mmoja wa watuhumiwa, Ram Sigh alijinyonga akiwa katika chumba chake gerezani Machi mwaka huu.

Hata hivyo hali ya mambo hapa nchini inaonekana kuwa tofauti, ni suala la kawaida kuona mawakili wakitetea hata wauza dawa za kulevya au watu wengine ambao wanaonekana wazi kufanya maovu yenye ushahidi kwa jamii.

Ni wakati wa Watanzania kuweka masilahi ya taifa mbele kwa kupigana vilivyo na watu wote ambao kwa namna moja ama nyingine wanachangia kurudisha nyuma maendeleo ya taifa.

 Makala haya yameandikwa na Julieth Kulangwa kwa msaada wa vyombo mbalimbali vya habari.

Bagamoyo na maeneo ya kihistoria yasiyojulikana

Sehemu ya lango la Mji wa Bagamoyo, wakati wa ukoloni.


Siku chache zilizopita nilitembelea Kitongoji cha Magomeni, mjini Bagamoyo, katika kitongoji hicho nilipiga picha vipande vya nguzo ambayo ni mabaki ya lango la mji huo.

Dereva wa bodaboda aliyenipeleka hapo nilimuuliza kama anaelewa chochote kuhusu kuta hizo mbili, lakini cha ajabu alisema hajui licha ya kuishi  Bagamoyo miaka mingi.

Baada ya hapo nilikutana na dada ambaye anasema amezaliwa na kuishi eneo la Magomeni, lakini hajui maana ya kuta hizo. Nilimwambia kijana kwamba enzi hizo, Bagamoyo ilipokuwa chini ya Wakoloni wa Kiarabu, eneo hilo palikuwa na lango likionyesha mtu anaingia mjini na kwa wenye nchi.

Misafara ya watumwa, wamisionari na wavumbuzi, wafanyabiashara, walipita katika lango hilo. Kuta  nyingine zilizokuwa upande mwingine wa barabara, zimepotea. Kuta nilizopiga picha ziko kwenye uwanja wa mtu. Zinaweza kupotea kwa kuharibiwa wakati wowote.

Pia kulikuwa na nguzo nyingine pale ‘top life bar’ lakini sasa imebaki moja, nyingine imepotea. Nilielezwa na wahifadhi kwamba eneo linalozunguka Caravan Serai, katika soko, na kule kituo cha mabasi kipya lilitumika kujenga kambi za watumwa. Lakini hakuna anayefahamu hilo.

Katika Idara ya Mambo ya Kale, inayoshughulikia masuala ya historia, hakuna maelezo yanayoonyesha eneo hilo kulikuwa na lango hilo. Hakuna kumbukumbu yoyote.

Nimekwenda Bagamoyo mara kadhaa, kila unapotembelea moja ya kivutio cha historia utapata habari tofauti, aidha itatofautiana na ya zamani, au itapotoshwa kidogo. Inafika mahali unashindwa kuelewa ukweli ni upi.

Baada ya kusoma kitabu cha Henry Morton Stanley anaeleza walipoanza safari walipumzika kwenye shamba la mama mmoja, Gonera wa Kihindi, nje ya Bagamoyo. Lakini safari hii niliambiwa Gonera alikuwa ni askari mlinzi aliyejengewa nguzo pale eneo la Mji Mkongwe na von Wisman mwaka 1898.

Inaonekana Bagamoyo ina maeneo mengi ya kihistoria ambayo hayajawekwa katika historia kuu. Na hili ni kosa la idara husika.

WATAKIWA KUTUNZA MIUNDOMBINU

Na John Banda, Dodoma

Wakazi wa kitongoji cha Msangalalee kata ya Dodoma Makulu Manispaa ya Dodoma wametakiwa kuilinda na kuitunza miundombinu ya maji safi iliyopo kwenye maeneo yao ili iweze kudumu kwa muda mrefu.

Kauli hiyo ilitolewa jana na mwenyekiti wa kitongoji hicho William Chacha wakati akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye kitongoji hicho.

Chacha alisema kumekuwa na tabia ya baadhi ya watu wasiokuwa waaminifu ambao huwa wanaharibu miundombinu ya maji kwa makusudi na kusababisha adha ya maji katika eneo hilo.

Alimtaka kila mtu kuwa mlinzi wa miundombinu ya hiyo ili huduma hiyo muhimu iwe endelevu kwa kupatikana kila wakati kwaa jili ya manufaa ya kila mmoja.

“Nimepata taarifa kuwa kuna watu wanang’oa mabomba ya maji na kwenda kuyauza kama vyuma chakavu, hilo ni kosa kisheria na kama tukikubaini tutakufikisha mahakamani kwa kosa la uharibifu wa miundombinu ya maji ambapo adhabu yake utaijua hukohuko mbele,” alisema Chacha.

Aliongeza, ni jukumu la kila mwananchi kulinda mabomba hayo ya maji safi kwani ndiyo chanzo pekee cha majisafi katika kitongoji hicho ambacho kimeanza kupata huduma ya majisafi mwaka huu tangu uhuru.

Akizungumza katika mkutano huo, mmoja wa wakazi wa kitongoji hicho Lesca Chedego aliipongeza mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira mjini hapa (DUWASA) kwa kuwafikishia huduma hiyo muhimu ya maji wakazi wa kitongoji hicho.

Kitongoji cha Msangalalee kimeanza kupata huduma ya majisafi tangu mwezi wa sita mwaka huu ambapo gharama za mradi huo ziligharamiwa na Duwasa kwa kuweka vituo (Domestic Points (DP)) 6 katika kitongoji hicho.

Mwisho

Hakimu achomwa kisu mahakamani



Shinyanga. Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo iliyopo eneo la Nguzo Nane, Kata ya Kambarage Mjini Shinyanga, Satto Nyangoha amejeruhiwa kwa kuchomwa kisu katika shavu lake la kushoto baada ya kutoa hukumu ya kesi ya wizi wa baiskeli.

Kitendo hicho kinadaiwa kufanywa na mlalamikaji katika kesi hiyo, Emmanuel Izengo (28), mkazi wa Tambukareli, Shinyanga baada ya kutokuridhishwa na hukumu iliyotolewa bila ya mshtakiwa, Daniel Makelezia, mkazi wa Lubaga Shinyanga na mdhamini wake, Marko Nkelezia kuwepo mahakamani.

Katika hukumu yake, Hakimu Nyangoha alisema mshtakiwa atakapopatikana atatumikia kifungo cha miaka miwili jela baada ya kupatikana na hatia ya wizi wa baiskeli hiyo aina ya Neria yenye thamani ya Sh150,000.

Awali, ilielezwa kwamba baada ya tukio hilo la wizi lililotokea Agosti Mosi, mwaka huu katika eneo la Nguzo Nane, mshtakiwa alikamatwa na kuwekwa mahabusu na kufunguliwa kesi namba 460 ya 2013 kabla ya kuachiwa kwa dhamana Agosti 23, mwaka huu huku kesi yake ikiendelea na pande zote mbili zilitoa maelezo.

Hata hivyo, baada ya kutoa maelezo, si mshtakiwa wala mdhamini wake aliyehudhuria mahakamani hapo licha ya kesi hiyo kusikilizwa mara mbili bila ya taarifa yoyote kabla ya hakimu huyo kutoa hukumu hiyo jana.

Kushambuliwa

Baada ya hukumu hiyo mlalamikaji alitoa shukrani na kuwashika mikono wote waliokuwamo mahakamani humo na kutoka nje.

Ilidaiwa kuwa baada ya dakika 15, Izengo alirudi mahakamani hapo na kudai kuwa ameleta risiti ya kumwonyesha hakimu thamani ya baiskeli yake alipoingia ndani ndipo kelele za Mshauri wa Baraza, Mary Wamba zikaanza kusikika akisema: ‘Njooni jamani hakimu kavamiwa anapigwa’.

Baada ya watu waliokuwa karibu kuingia katika ofisi ya Mahakama hiyo walikuta hakimu ameshacwhomwa kisu katika shavu la upande wa kushoto huku akivuja damu nyingi huku mtuhumiwa huyo akiendelea kumshambulia. Baada ya tukio hilo, wasamaria wema walimpeleka hakimu huyo katika Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga ambako alilazwa kwa matibabu.

Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Evarist Mangala alisema mtuhumiwa alikamatwa mara baada ya tukio hilo kusubiri hatua za kisheria dhidi yake.

Balozi Msuya : Vijana acheni kukimbilia Sauzi si peponi

Balozi Radhia Msuya 


Pretoria. Kwa siku za karibuni limetokea wimbi kubwa la vijana  wa Kitanzania kukimbilia nchi mbalimbali duniani ikiwamo Afrika Kusini kwa madai ya kusaka maisha bora.

Baadhi ya vijana hao wamekuwa wakikamatwa na hata kurudishwa nchini baada ya kukosa uhalali kisheria wa kuendelea kuishi katika nchi hizo.

Wengine kati yao wamejikuta matatani kwa kuhusishwa na usafirishaji wa dawa za kulevya pamoja na maovu mengine baada ya  kuingia katika nchi hizo kwa njia halali na zisizo halali.

Kwa upande wa Afrika Kusini, baadhi ya vijana hao wemeamua kuhamishia shughuli zao za kibiashara nchini humo.

Balozi wa Tanzania nchini humo, Radhia Msuya  anasema vijana wengi wanadanganyika kwa kufikiri kuwa maisha katika nchi hiyo ni rahisi na kuwa baada ya kufika huko mambo yatakuwa rahisi na kinyume chake mambo huwawia magumu na baadhi yao kuhitaji msaada wa kurudishwa nyumbani.

Vijana 200 kwa mwezi

Balozi Msuya anasema kila mwezi wastani wa vijana  200 hurudishwa nyumbani Tanzania kutoka nchini humo kutokana na sababu mbalimbali wakiwamo wale walioingia katika nchi hiyo bila vibali.

 ‘’Huku siyo peponi, maisha bora yanafanyiwa kazi kama ilivyo huko nyumbani. Kila mwezi tunarudisha nyumbani vijana  200 wanaokamatwa mitaani hapa wakiuza  bidhaa ndogo ndogo huku wengi wao wakiwa hawana vibali,’’ anasema Balozi Msuya.

 Anasema shughuli ndogo ndogo za biashara wanazofanya vijana hao kutoka Tanzania haziwawezeshi kumudu gharama kubwa za maisha nchini humo na baadhi yao hudaiwa kujihusisha na vitendo vya uhalifu, ikiwemo matumizi ya dawa za kulevya.

Aidha, balozi  huyo  anawataka vijana wasiamini kuwa majibu yote ya changamoto zote zinazowakabili yanapatikana serikalini.

Anasema  baadhi ya majibu ya changamoto hizo yako mikononi mwao na utatuzi wake siyo lazima kukimbilia nchini humo.

 Anasema ni kweli  Afrika Kusini imepiga hatua kubwa kimaendeleo katika sekta mbalimbali ikiwamo maendeleo  ya kiuchumi, ingawa  pia yapo matatizo mengi  ambayo vijana hukumbana nayo baada ya kufikiri kwamba kukimbilia nchini humo litakuwa ni suluhisho la matatizo yote waliyoacha nyumbani.

 

“Ni kwamba  changamoto kubwa iliyopo ni vijana wetu kuacha kukimbilia nchini humu kwa dhana kwamba ‘wataukata’ tena bila ofisi za ubalozi wetu kuwa na taarifa za ujio wao. Baadhi ya vijana hao kupata matatizo ndipo hukumbuka  hukimbilia katika ofisi  yetu kwa ajili ya kupatiwa msaada,” anaeleza Balozi Msuya.

 Kifo cha Mangwea

Mathalan, Balozi Radhia Msuya  anasema ofisi za ubalozi wake hazikuwa na taarifa za ziara au safari ya msanii maarufu wa Tanzania, Albert  Mangwea kwenda nchini humo miezi michache iliyopita na hata alipofariki ghafla wao walipata wakati mgumu sana katika kufuatilia na kupata taarifa zake.

 Anasema baada ya taarifa za kifo cha msanii huyo kusambaa kwenye mitandao watu wengi  kutoka Tanzania  walipiga simu katika ofisi za ubalozi mjini Pretoria ili wapewe ukweli wa tukio hilo,ilihali ofisi za ubalozi hazikuwa na taarifa za msanii huyo kuwamo nchini humo.

Balozi huyo anabainisha kuwa huo ni mfano mmoja wa Watanzania wanaoingia nchini humo bila taarifa.

Anaeleza kuwa hivi sasa ni vigumu kufahamu Watanzania wanaoingia na kutoka nchini humo baada ya kufutwa kwa viza kati ya nchi hizo na hivyo kukata mkondo wa mawasiliano ambao ungewalazimisha kufika katika ofisi za ubalozi.

‘’Kifo cha Ngwea (Albert) kwa upande wetu kimetupa uzoefu, tunakosa  taarifa kamili za Watanzania wote wanaofika na kuondoka hapa nchini baada ya kufutwa kwa viza. Hata hivyo, hilo haliondoi wajibu wetu kama ofisi za ubalozi,’’ anabainisha Balozi Msuya.

 Anatahadharisha kuwa ni muhimu raia yeyete anayefika nchini humo kutoa taarifa kwenye ofisi za ubalozi huo ili kujenga uwezekano wa kupata msaada haraka endapo atapata matatizo tofauti na sasa ambapo wengi wao hawaoni ulazima wa kufanya hivyo.

Mtazamo wa Bushoke

Naye Maxmilian Bushoke, msanii Mtanzania anayefanya shughuli za muziki jijini Johannesburg anasema vijana wengi wanakimbilia katika nchi hiyo kubwa kiuchumi barani Afrika wakidhani kuwa nyumbani  hakuna mazingira rafiki ya kazi wanazofanya.

Anasema wapo vijana wengi kutoka nyumbani katika mitaa mbalimbali ya Jiji la Johannesburg wanaofanya shughuli ndogo ndogo za biashara na kukiri wengi wao kuhusishwa na matukio mbalimbali ya uhalifu ikiwemo matumizi ya dawa za kulevya. 

Utalii Afrika Kusini

 Akizungumzia nafasi ya vivutio vya utalii nchini Afrika Kusini, Balozi Radhia Msuya anasema kuwa miongoni mwa kazi za ubalozi huo ni kutangaza vivutio vilivyopo Tanzania na fursa za uwekezaji zilizopo ili kuongeza idadi ya watalii.

 Anasema kupitia ofisi za  ubalozi huo wamefanikiwa kushawishi watalii wengi nchini humo kutembelea Tanzania  hasa maeneo mbalimbali ya vivutio kama  Hifadhi za Taifa na kuwa matarajio ni kufanya vizuri zaidi kuwashawishi watalii wengi zaidi kutoka Afrika Kusini kutembelea nchi yetu.

 Hata hivyo, Balozi  Msuya anasema kuwa Tanzania haijapiga hatua kubwa katika masuala ya kuhifadhi mambo ya kale ikilinganishwa na nchi hiyo ya kusini mwa Afrika ambayo inapata fedha nyingi za utalii ikiwa ni matokeo ya kuhifadhi vyema maeneo muhimu ya  kihistoria. Anasema kwamba yapo mambo ambayo Watanzania wanafikiri ni madogo ingawa yana umuhimu mkubwa katika historia ya nchi.

Anasema kuwa yanayofikiriwa kuwa madogo ni vivutio vikubwa ambavyo huingiza fedha nyingi katika nchi zinazotunza vizuri historia. ‘’Wapo ambao hawana hata kumbukumbu ya cheti cha darasa la saba,hapo ndipo uhifadhi unapoanzia,kuna  vijana wengi ambao hawajui mambo muhimu  yanayohusu historia ya nchi yao,’’ anabainisha Balozi Msuya.

 Anatoa mfano wa eneo la Mnara wa Saa jijini Dar es Salaam analosema kuwa ni eneo muhimu katika historia ya nchi kwani hapo ndipo lilitolewa tamko rasmi  la kutangaza jiji hilo kuwa makao makuu ya nchi, lakini anahoji ni wangapi wanaojua jambo hilo. Hata hivyo, balozi huyo anasema eneo hilo limesahauliwa na hazionekani  dalili za kulihifadhi na kutangaza ‘mnara wa saa’ kama eneo muhimu la historia ya nchi.

Anasema eneo hilo limeendelea kuachwa kama lilivyo huku likisahauliwa na historia ya nchi, jambo ambalo ni hatari.

“Mambo mengi  yamesahaulika. Kwa mfano, njia alipopita Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere kwa mguu wakati wa matembezi ya kuunga mkono Azimio la Arusha akitokea kijijini Butiama hadi Mwanza hazijulikani. Hakuna utambulisho wa  tukio hilo la kihistoria katika maeneo  aliyopita,” anaeleza na kutoa changamoto kwa mamlaka za umma nchini kushughulikia jambo hilo kama kivutio cha utalii.

Tanzania yajitosa kumsaidia Ruto

 

Serikali ya Tanzania, imeiomba Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kuruhusu Makamu wa Rais wa Kenya, William Ruto kutohudhuria baadhi ya mashauri ya kesi yake ili kuweza kutimiza majukumu mengine ya kiserikali.

Mwanasheria Mkuu wa Tanzania, Jaji Fredrick Mwita aliandika barua kwenda ICC Jumatatu wiki hii akitetea hoja ya Ruto kutaka asihudhurie baadhi ya vikao vya kesi hiyo.

Katika barua yake, Jaji Werema alisema kuruhusu Ruto kutohudhuria baadhi ya vikao vya kesi kutaimarisha ushirikiano baina ya ICC na washirika.

Hata hivyo, maombi hayo yanayotaka Ruto kuruhusiwa kutohudhuria kesi hiyo binafsi yamesimamishwa baada ya mwendesha mashtaka wa ICC, Fatou Bensouda kuyawekea pingamizi na sasa yanasubiri uamuzi wa majaji.

Hii ni mara ya pili kwa Tanzania, kuwasiliana na ICC kwani iliwahi kuwasilisha ombi la kutaka kesi hiyo ya kina Ruto isikilizwe Tanzania au Kenya.

Hata hivyo, mpango huo ulikwama baada ya majaji kuupinga kwa kura za hapana.

Mwandishi Sang ajitetea

Mwandishi wa habari wa kituo cha KASS FM Joshua Arap Sang, amekamilisha ungwe ya kwanza ya utetezi wake kwenye Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) na kueleza kuwa hakuhusika kwa namna yoyote kuchochea machafuko yaliyojiri baada ya uchaguzi nchini Kenya.

Sang aliwasilisha utetezi wake katika hali ya kujiamini huku akionyesha sura yenye matumaini na kuiambia mahakama kuwa, kesi inayomkabili imetengenezwa ili kukatiza ndoto yake ya kuwa mtangazaji bora duniani .

Mwandishi huyo ambaye anatetewa na mawakili wanaoongozwa na Wakili Katwa Kigen, alipangua hoja zilizowasilisha na upande wa mashtaka kwa kutumia historia ya maisha yake aliyoyaelezea kuwa ni ya kumcha Mungu na uadilifu.

Kama ilivyo kwa washtakiwa wengine, Rais Uhuru Kenyatta na Naibu wake William Ruto, Sang anadaiwa kuratibu na kupanga mashambulizi na kusababisha zaidi ya watu elfu moja kupoteza maisha.

Pia anadaiwa kuendesha kampeni ya uchochezi kupitia vipindi mbalimbali vya redio baada ya matokeo ya uchaguzi mkuu wa 2007.

Mbele ya jopo la majaji wanaosikiliza kesi hiyo, Sang alisema historia ya maisha yake inaeleza vyema namna alivyokuwa msaada kwa jamii, ikiwamo kushiriki kikamilifu shughuli za kanisa hivyo kutuhumiwa kuwa alihusika kwenye mauwaji ni dhihaka kubwa kwake.

“Kwanza nianze kwa kumshukuru Mungu ambaye kwake yeye nimepata nguvu na kusimama hapa. Nafahamu fika ipo siku mahakama hii itasimama katika haki na kuniachia huru. Itamwachia huru mwandishi wa habari.

“Lakini pia napenda niiarifu mahakama hii kuwa mimi ni kiongozi wa kwaya tena nategemewa sana na wenzangu, sasa kuambiwa kuwa nimeratibu mauaji ya raia ni jambo linalonisononesha sana tena limenivuruga mno,” alieleza Sang.

Katika kile kilichoonekana kama njia ya kuupa nguvu utetezi wake, Sang mbali ya kuelezea uzoefu wa kazi yake lakini alirudia mara kadhaa kutamka maneno yaliyotafsiri hisia zake dhidi ya kesi hii.

“Kusema kweli haya mashtaka yamenisononesha na kunivuruga. Mimi ni mzazi na pia ni mume mwema, itakuwaje sasa nithubutu kufanya jambo hili la kuua wenzangu, haiwezekani. Nimesikitika na kusononeka sana”.

Uzoefu wake

Baadaye aligeukia kipengele kilichohusu uzoefu wa kazi yake ambapo alitetea utendaji wake akisema; wakati wote alikuwa akifanya kazi kwa kuzingatia miiko na madili.

“Mimi ni mtangazaji wa siku nyingi tena nimefanya kazi hii katika vituo zaidi ya vitatu ambavyo vyote ni vya kidini, sasa huko kote nisifanye hilo la kuchochea mauaji nije kulifanya hapa Kass FM. Hiyo siyo kweli kabisa na hii kesi imeletwa kwa ajili kunivurugia tu safari yangu ya kuendelea kuwa mtangazaji.

Aliongeza: “Potelea mbali najua Mungu yupo na ataendelea kunipigania. Natambua kuwa mimi nilizaliwa kuwa mtangazaji na hadi leo nitabakia kuwa hivyo.”alisema

Aliiambia mahakama hiyo kuwa kazi ya utangazaji alianza kuipenda alipokuwa kijana mdogo na wakati fulani alilazimika kufuatilia matangazao yaliyokuwa yakirushwa na kituo cha BBC kwa ajili ya kujifunza na kupata taarifa za dunia.

“Waheshimiwa majaji mimi ni msikilizaji mzuri wa redio na kituo nilichokuwa nikikifanyia kazi Kass FM kinasikika kimataifa, hata hapa Netherland mimi nasikiliza redio hii, hivyo nina ufahamu wa kutosha wa kazi hii.

Napenda tu niseme haya mashtaka hayana ukweli wowote kabisa,”alisema.

Kuhusu vipindi alivyokuwa akiviendesha ambavyo vinadaiwa kupendelea kambi ya ODM, Sang alipuuza hoja hiyo kwa kueleza kuwa, wakati wa kampeni vyama vya siasa ndivyo vinavyolipia matangazo kwa ajili ya kutangaza sera zao.

“Pale Kass FM mimi ni mtu mdogo kabisa, sina uwezo wa kuamua jambo lolote lile mbali ya kufuata utaratibu uliowekwa na mmiliki wa kituo, lakini pia kusema mimi nilipendelea kambi ya ODM kwa kuwapa vipindi vingi hili siyo kweli kabisa, lazima tujue kwamba wakati wa kampeni vituo vingi huuza muda kwa wanasiasa ili watangaze sera zao ndivyo ilivyokuwa kwetu,” alieleza.

Sang pia alikanusha tuhuma za kuendesha vipindi vya redio vinavyodaiwa kurushwa kwa kipindi cha siku tatu kuanzia mwanzoni mwa Januari, 2008 vilivyokuwa vikiwahimiza wananchi wa kabila la Kilinjini kuanzisha machafuko.

Wanusurika kufa kwa pombe


Iringa. Zaidi ya watu 19 katika Kijiji cha Imega, katika Wilaya ya Kilolo, wamenusurika kufa baada ya kunywa pombe ya kienyeji inayodhaniwa kuwa na sumu.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa, Ramadhani Mungi alisema tukio hilo lilitokea juzi wakati watu hao walipokwenda kuhudhuria sherehe iliyoandaliwa na mzee mmoja. Kwa mujibu wa kamanda huyo, sherehe hizo zilikuwa ni za kumuaga binti yake aliyekuwa akiolewa.

Alisema baada ya kazi hiyo, watu hao walianza kunywa pombe ya kienyeji na ilipofika jioni watu 19 walipatwa na ugonjwa wa tumbo. Kamanda huyo alisema baadaye watu hao walipelekwa katika Zahanati ya kijiji hicho kwa matibabu.

Alisema wakati wakiendelea kupata matibabu ,mmoja wa watu hao, alizidiwa na kukimbizwa katika Hosptali ya Itunda kwa matibabu zaidi. Alisema uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa huenda pombe walioitumia ilikuwa na sumu.

“Pombe hiyo inatokana na mahindi na inasemakana mahindi hayo yalikuwa na dawa. Tunafanya uchunguzi,” alisema Mungi.

WAHAMIAJI HARAMU 133 MBALONI JIJINI DAR ES SALAAM


Jijini Dar es Salaam hekaheka za wahamiaji haramu zimeendelea, baada ya watu 133 kutoka mataifa mbalimbali kutiwa mbaroni.

Hatua hiyo, inatokana na msako mkali uliopewa jina la ‘Endelevu’ unaoendelea katika maeneo mbalimbali.

Akizungumza na MTANZANIA ofisini kwake mwishoni mwa wiki iliyopita, Naibu Kamishna wa Idara ya Uhamiaji na Msemaji Mkuu, Abbas Irovya, alisema msako ambao ulianza mwanzoni mwa mwezi huu umekuwa na mafanikio.

Alizitaja nchi wanazotoka na idadi yao kwenye mabano kuwa ni Burundi (41), Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (30), Kenya (11), Uganda (6), Pakistan (3), Somalia (7), Nigeria (4) na Cameroon (1).

Nchi nyingine ni Afrika Kusini (1), Malawi (11), Rwanda (44) na Msumbuji (7).

Uchunguzi uliofanywa na MTANZANIA mjini Dar es Salaam katika maeneo ya Mwananyamala, Mikocheni, Tegeta, Msasani, Sinza na Temeke umebaini kuwapo na idadi kubwa ya wahamiaji haramu.

Juzi katika eneo la Mikocheni B, MTANZANIA ilishuhudia raia kadhaa wa Malawi wakiwa wamekusanyika kwa ajili ya kufanya kikao cha dharura, kwa ajili ya kuchangishana fedha waondoke nchini.

Mmoja wa raia hao (jina tunalo), alisema hivi sasa hawaishi kwa amani hata kidogo kutokana na jamaa zao wengi kukimbia makazi na kutelekeza familia zao.

“Tunaishi maisha ya shaka mno, naona ni bora nitafute mtu nimuuzie vyombo vyangu ili nirudi nyumbani haraka, maisha Malawi ni magumu mno tofauti na Tanzania,” alisema

Chanzo: Mtanzania