Wasaudia wanne mbaroni, FBI watua Arusha

 
Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal akimjulia hali Restuta Alex (50), aliyelazwa katika Hospitali ya Mount Meru Arusha, baada ya kujeruhiwa katika mlipuko wa bomu uliotokea juzi. Kushoto ni Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Alex Malasusa na Kulia ni Mkurugenzi wa Maelezo, Assah Mwambene.

Dodoma/Arusha. Wakati maofisa wa Shirika la Upelelezi wa Marekani (FBI) wametua Arusha, raia wanne wa Saudi Arabia na Watanzania wawili wamekamatwa kwa tuhuma za kuhusika kulipua bomu lililoua watu wawili na kujeruhi wengine 61 wakati wa ufunguzi wa Kanisa la Mtakatifu Joseph Parokia ya Olasiti.

Waliofariki dunia ni Regina Longino Kurusei (45), mkazi wa Olasiti na James Gabriel (16), ambaye alifariki usiku wa kuamkia jana.

Tukio hilo lilitokea wakati Balozi wa Vatican na Mwakilishi wa Papa nchini, Francisco Montecillo Padilla alipokuwa akizindua kanisa hilo.

Akitoa maelezo kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda jana, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo alisema raia hao wa Saudi Arabia walikamatwa jana asubuhi baada ya tukio wakiwa kwenye gari wakielekea Kenya kupitia Namanga.

Mulongo alisema raia hao wa kigeni waliingia nchini Jumamosi iliyopita na siku iliyofuata ndipo kukatokea ulipuaji huo. Alisema lengo la shambulizi hilo lilikuwa kumdhuru Askofu Padilla.

“Mtu ambaye tulimkamata jana (juzi Jumapili) ndiye aliyesaidia kuwapata watu hawa wa Saudi Arabia na Watanzania hao,” alisema Mulongo.

Mulongo alisema maofisa wa FBI walifika jana saa tano asubuhi ili kusaidiana na Polisi na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), katika uchunguzi wa tukio hilo.

Maofisa hao wa FBI walikuwa Zanzibar ambako walikuwa wanachunguza kifo cha Padri Evaristus Mushi ambaye aliuawa Februari 17, mwaka huu.

Hii itakuwa mara ya pili kwa wageni kuhusishwa na matukio ya ugaidi nchini baada ya mwaka 1998 wakati raia kadhaa wa Misri wakiongozwa Fazul Abdulla waliposhirikiana na Watanzania kadhaa akiwamo Ahmed Ghailani kulipua ubalozi wa Marekani nchini na ule wa Kenya. Ghailani anatumikia kifungo cha maisha nchini Marekani wakati Fazul aliuawa Somalia mwaka 2011.

Tamko la Serikali

Akitoa tamko la Serikali bungeni jana, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi alimtaja mmoja wa watuhumiwa wanaoshikiliwa kuhusika na tukio hilo kuwa ni Victor Calisti Ambrose (20), mkazi wa Kwa Mrombo Arusha ambaye ni dereva wa bodaboda. Alisema kijana huyo ndiye anayetuhumiwa kurusha bomu hilo.

Waziri Nchimbi alitoa onyo kali kwa wanasiasa wanaopandikiza chuki za kidini miongoni mwa Watanzania na kuishutumu Serikali kutokana na matukio kama hayo. “Kuna wanasiasa ambao wanaona masilahi yao ni muhimu kuliko maisha ya Watanzania, masilahi yao ni muhimu kuliko utulivu wa Watanzania na masilahi yao ni muhimu kuliko umoja wa Watanzania.”

JK akatiza ziara, Bilal atoa ahadi

Rais Jakaya Kikwete, amekatiza ziara yake ya kiserikali nchini Kuwait ili kurejea nyumbani kutokana na shambulio la bomu kwenye kanisa hilo.

Taarifa ya Ikulu imesema jana kwamba Rais Kikwete amelazimika kukatiza ziara hiyo na kurejea nyumbani mara moja ili kuwa karibu na wafiwa pamoja na wale waliojeruhiwa katika shambulio hilo la kigaidi.

Makamu wa Rais, Dk Gharib Bilal ameahidi kuwa Serikali itahakikisha wote waliohusika na tukio hilo wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya dola.

Balozi wa Papa atoa tamko

Askofu Padilla ambaye jana alitembelea majeruhi katika Hospitali ya Mkoa, Mount Meru, alieleza kustushwa na tukio hilo na kusema hakutarajia kitu kama hicho kutokea wakati wa shughuli hiyo wakati Watanzania wakijulikana ni watu wa amani.

Alilaani tukio hilo na kuvitaka vyombo vya usalama kufanya uchunguzi ili kubaini ukweli.

Kanisa Katoliki Arusha

Kanisa Katoliki, Jimbo Kuu la Arusha jana liliitaka Serikali iwataje waliohusika na tukio hilo la kigaidi huku likiwataka waumini wake kutolipiza kisasi.

“Msimamo wa kanisa katika hili, ni kuwataka waumini wasilipize kisasi kama ambavyo alisema Yesu Kristo kuwa msilipize kisasi, muwe tayari kushinda ubaya kwa wema,” alisema Askofu Josephat Lebulu na kuongeza:

EU

Jumuiya ya Umoja wa Ulaya (EU), imetaka kuharakishwa kwa uchunguzi wa tukio hilo na kuonya kuwa matukio kama hayo yanaweza kulitumbukiza taifa kwenye machafuko.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Balozi wa Umoja huo nchini, Filiberto Ceriani-Sebregondi alisema Tanzania inapaswa kufahamu kwamba pasipo kujenga, kuendeleza na kusisitiza utamaduni wa kuvumiliana, hali inaweza kuwa mbaya zaidi kwa siku za usoni.

Ripoti yabaini mwandishi mmoja huuawa duniani kila baada ya siku 5

Askaro Polisi wakiwa katika eneo alipouawa Mwandishi wa Habari, Daudi Mwangosi kwa kulipuliwa na bomu la machozi mwaka jana.

Dar es Salaam. Mwishoni mwa  wiki tasnia ya habari ilifanya kumbukumbu ya Siku ya Uhuru wa Habari  huku taarifa zikionyesha kuwa kwa miaka kumi iliyopita, wastani wa mwandishi mmoja kuuawa kila baada ya siku tano katika maeneo mbalimbali duniani.             

Ripoti iliyoandaliwa na jumuiya ya kulinda usalama wa waandishi wa habari duniani (CPJ)  inaeleza kuwa tangu mwaka 1992  mpaka 2013, waandishi 982 wameuawa.

Sababu za mauaji hayo zinatajwa  kuwa ni mazingira ya utekelezaji wa kazi zao.

Ripoti ya CPJ inaonyesha nchi za Afrika na Uarabuni zinaongoza katika utekelezaji wa mauaji hayo huku Somalia ikiripotiwa kuuawa waandishi 50 katika kipindi hicho.
Nchi kubwa zenye idadi ndogo ya mauaji hayo ni Uingereza(1), Ufaransa(1), China (2), Japan (1)na  Hispania(1). Tanzania ni moja kati ya nchi zilizotajwa na kuingia katika ripoti ya kumbukumbu hiyo duniani kutokana na kifo cha mwandishi wa habari wa kituo cha Channel Ten mkoani Iringa, Daudi Mwangosi.

Pia, mwanahabari Issa Ngumba wa Radio Kwizera aliuawa kule Kakonko, Mkoani Kigoma.

Kutokana na matokeo hayo, wadau mbalimbali wa masuala ya habari nchini wametoa maoni yao  juu ya mwenendo wa uhuru wa vyombo vya habari nchini wakisema uhuru huo sasa umetiwa kitanzini.

MCT
Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Kajubi Mukajanga amesema katika kipindi cha hivi karibuni usalama kwa waandishi wa habari umepungua kutokana na kuwapo kwa matukio ya vitisho visivyotarajiwa miongoni mwao.

Mukajanga alisema mbali na mauaji ya Mwangosi, kuna baadhi ya vitisho vimetolewa kwao wakiwa katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Matukio ya utekaji nyara japokuwa hatujapata uthibitisho lakini hali hiyo imeondoa taswira ya nchi na kushusha heshima yake kimataifa,” alisema Mukajanga.

Mukajanga alisema matukio hayo yamesababishwa na hali ya kuibuka kwa makundi ya kisiasa na kidini katika kipindi cha hivi karibuni hatua iliyochangia mwandishi kunyimwa uhuru na kujengewa dhana ya kuegemea upande mmoja katika uandishi wa habari zake hususan zinazogusa makundi hayo.

“Kwa mazingira hayo mwandishi wa habari lazima atakuwa na wakati mgumu sana, hata kama ataandika ukweli bado atakuwa amesababisha madhara au kuharibu masilahi ya upande mwingine,” anasema Mukajanga.

Hata hivyo, Mukajanga alitoa mapendekezo yake akiwataka waandishi wan habari kusimamia maadili ya kazi zao ili jamii itambue ukweli hata kama wataendelea kupigwa vita.

 

TMF  
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania (TMF), Erenest Sungura alisema kutokana na usalama wa mwandishi wa habari kupungua hapa nchini, Serikali inatakiwa kuangalia changamoto za kimazingira zinazochangia madhara hayo.

Sungura alisema inawezekana moja ya sababu ni pamoja na sheria zinazonyima uhuru wa kuandika habari fulani hivyo mwandishi hujikuta akilazimisha kuandika ukweli katikati ya ukiukwaji wa sheria zinazombana.

“Kuna sheria zinazowanyima uhuru wa kuandika mambo mengine zifanyiwe mabadiliko,” alisema.

Hata hivyo, Sungura anatoa wito akiwataka wamiliki wa vyombo vya habari kutengeneza mazingira ya ulinzi wa kutosha kwa waandishi wao pale wanapokuwa wanafanya kazi za uchunguzi.

“Wahariri waangalie suala hilo kwa sababu mimi napokea simu karibu tano kwa mwezi za waandishi wakieleza kupewa vitisho,” anasema.
Mbali na hilo, Sungura anawataka pia waandishi wazingatie maadili ya kazi zao ili kujenga taswira ya ubora wa taaluma yao ili kujiweka huru na kupunguza uadui miongoni mwa jamii zenye makundi.   

Taswa
Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo nchini (Taswa),  Juma Pinto anasema tofauti za makundi ya kisiasa ndiyo imekuwa chanzo cha mwandishi wa habari nchini kukumbwa na hatari ya usalama wake pale anapokuwa akitekeleza majukumu yake.

“Makundi ya kisiasa  ndiyo tatizo zaidi, kwa nini hatusikii kwenye michezo  au burudani,” alisema.

Pinto anasema kutokana na mazingira magumu yaliyopo kwa sasa, ameshauri waandishi kuwa na umoja na msimamo mkali pale inapotokea mwandishi ameingia kwenye matatizo ya vitisho, kutekwa au kuuawa.

“Mbali na msimamo wetu Serikali pia inatakiwa kuangalia sheria kandamizi kwa mwandishi wa habari, Katiba yenyewe inamtambua mmiliki wa chombo na sio mwandishi, yaani mwandishi wetu hapa nchini ni sawa na mtoto aliyetelekezwa, hana sehemu yoyote inayomtambua,” anasema Pinto.

Hali katika nchi nyingine
Mbali na taarifa hizo, hali si salama kwa nchi nyingine ambapo shirika la waandishi wa habari wasio na mipaka duniani liliripoti kuwa mwaka 2012 ulikuwa ni mwaka wa maafa zaidi kwa waandishi wa habari kote duniani ukilinganisha na miaka iliyopita.

Somalia ambayo haina serikali thabiti iliripotiwa kufanya mauaji ya waandishi 18 na Pakstan waandishi 10.

Katika ripoti hiyo ya Desemba 19,  2012,  ofisa wa shirika hilo, Ulrike Gruska anasema  waandishi 88 waliuawa wakati wakiripoti kazi zao kutoka maeneo yenye vita na mashambulizi ya mabomu huku sababu zikielezwa kuwa ni pamoja na mazingira ya kutatanisha, makusudi na uhasama kutoka kwa baadhi ya wanasiasa.

 

Ripoti hiyo inasema mpaka sasa kuna jumla ya waandishi wa habari 65 wameuawa nchini Syria mwaka huu, wakati wanatekeleza majukumu yao, huku 21 wakiswekwa rumande na makundi ya watu ama wapiganaji nchini humo.

Nchini Mexico, waandishi wanaishi katika maisha ya hatari,hasa wanapokuwa wanaripoti kuhusu uhalifu, usafirishaji wa dawa za kulevya na uhusiano kati ya viongozi wa magenge ya wahalifu na wafanyakazi wa umma.

Taarifa nchini humo zinasema kuna idadi ya waandishi sita wameuawa tangu Januari mwaka huu.

Mbali na nchi hiyo, Brazil pia imetajwa kama mojawapo ya nchi hatari kwa waandishi wa habari kutokana na vita inayofanywa dhidi ya wafanyabiashara wa dawa za kulevya.

Matukio ya unyanyasaji  
Katika hatua nyingine, hali imeonyesha wasiwasi baada ya kuongezeka kwa idadi ya waandishi duniani waliofungwa jela mwaka huu. Ripoti hiyo inasema zaidi ya waandishi na wana ‘blogi’ 1,000 walikamatwa mwaka huu huku zaidi ya 2,000 wakipewa vitisho.

Hatari; Bomu larushwa kanisani Arusha, mmoja afariki

 

Derick Cyprian akiangaliwa na baba yake katika Hospitali ya Mount Meru jana baada ya kujeruhiwa na bomu.

Arusha.Mtu mmoja amefariki dunia na wengine 59 kujeruhiwa akiwamo Balozi wa Vatican na Mwakilishi wa Papa nchini Tanzania, Askofu Mkuu Francisco Montecillo Padilla jana asubuhi baada ya mtu asiyejulikana kurusha bomu wakati wa sherehe ya uzinduzi wa Jengo la Kanisa la Parokia ya Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Olasiti, Arusha.

Miongoni mwa majeruhi, imeelezwa kuwa wanne ni mahututi.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas amelielezea kuwa tukio hilo kuwa ni la kigaidi hasa kutokana na kumlenga Balozi wa Papa nchini na kwamba mtu mmoja anashikiliwa akihusishwa nalo.

Wataalamu wa mabomu wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) wanachunguza aina ya bomu lililotupwa lakini uchunguzi wa awali unaonyesha lilikuwa limetengenezwa kienyeji.

Ilivyokuwa

Watu walioshuhudia tukio hilo wanasimulia kuwa bomu hilo lilirushwa yapata saa nne asubuhi wakati mgeni rasmi akijiandaa kufungua jengo la kanisa baada ya ujenzi wake kukamilika.

Shambulio hilo lilitokea wakati balozi huyo akiwa amesimama na mwenyeji wake, Askofu Mkuu, Josephat Lebulu, mapadri na watawa kutoka mashirika mbalimbali ya Jimbo Kuu la Arusha kwa ajili ya kukata utepe wa uzinduzi.

Kamanda Sabas alisema mtu aliyerusha bomu hilo alitokea nyuma ya kanisa hilo la ghorofa na kurusha bomu hilo kwa mkono wa kulia... “Alifanya jitihada za kupenya ili awafikie viongozi lakini alishindwa kutokana na wingi wa waumini waliokuwapo kwenye eneo hilo.”

Padri Moses Mwaniki aliyemshikia Balozi Padilla maji ya baraka yaliyotumika kubariki kanisa hilo, alisema kilichosaidia bomu hilo kutomfikia mwakilishi huyo wa Papa ni kutua mgongoni mwa mmoja wa waumini na kuanguka chini kabla ya kulipuka na kujeruhi watu.

“Ingawa hatuwezi kusema kwa uhakika, tunaamini mlengwa mkuu alikuwa mgeni wetu, Balozi Askofu Mkuu Padilla. Tunatakiwa kuliombea sana Taifa liondokane na matukio mabaya kama haya,” alisema Padri Mwaniki.

Baada ya tukio hilo, Balozi Padilla, Askofu Lebulu na viongozi wa kanisa hilo waliondolewa na kuhifadhiwa katika moja ya vyumba vya kanisa hilo kabla ya kutolewa kwenye eneo hilo yapata saa 5.30 asubuhi chini ya ulinzi mkali wa polisi.

Msemaji wa Kanisa Katoliki, Jimbo Kuu la Arusha, Padri Festus Mangwangi alisema aliyerusha bomu hilo alishuhudiwa na mtoto mdogo aliyekuwapo kanisani hapo.

 

“Kwa mujibu wa maelezo ya mtoto huyo, mtu huyo alikuwa amevaa kanzu nyeupe pamoja na koti la mvua lenye rangi ya kahawia na alikimbia mara baada ya kulirusha katikati ya watu. Ametusimulia kuwa mtu huyo baada ya kurusha bomu lile alikimbia na kuwahadaa watu kwa kuita ‘mwizi mwizi mwizi…’ akionyesha mbele kama kuna mtu anayemfukuza jambo lililowazubaisha watu lakini mtoto aliyemwona akirusha bomu aliwaeleza kuwa ndiye mhusika.”

“Waliomshuhudia mhusika akikimbia wanasema walishindwa kumwona mwizi aliyekuwa akimfukuza na hivyo kubaki wakimkodolea macho, hali iliyomfanya atokomee katikati ya nyumba za watu,” alisema Padri Mangwangi, ambaye aliongeza kuwa katika kipindi hicho kulikuwa kuna mkanganyiko mkubwa kutokana na bomu kulipuka na mtu huyo kudai kuna mwizi.

Mwenyekiti wa Parokia ya Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Julius Mbaga ambaye mkewe, Concesa (42), ni mmoja wa majeruhi, alisema ni kudra za Mwenyezi Mungu pekee ndizo zimeepusha madhara na maafa makubwa.

Kifo na majeruhi

Aliyefariki ametambuliwa kuwa ni Regina Losioki (46), ambaye alikuwa anaimba kwaya katika kanisa hilo. Alifariki baada ya kufikishwa katika Hospitali ya St. Elizabeth, Arusha.

Mamia ya watu jana walifurika katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru kushuhudia watu waliokuwa wakifikishwa hapo kutoka katika eneo la tukio.

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa, Dk Frida Mokiti alisema majeruhi 41 walikuwa wamelazwa Mount Meru, 16 walikuwa Hospitali ya St Elizabeth huku mmoja akiwa katika Hospitali ya Selian na mwingine Hospitali ya Kaloleni... “Kuna mgonjwa mmoja, ambaye amepelekwa Hospitali ya Rufaa ya KCMC (Moshi) kwa matibabu zaidi.”

Waliojeruhiwa ambao majina yao yalibandikwa katika ukuta wa Hospitali ya Mount Meru ni Christopher Raymond (10), Consensia Mbaga (53), Deborah Joachim (24), Elizabeth Isdori (24), Bertha Cosinery (49), Anna Didas (52), Edda Ndowo(77), Derick Cyprian (8), Faustine Andrea (35), Mary Okech na Neema Daud (13).

Alex Arnold, Agripina Alex (9), James Gabriel (16), Loveness Nelson (17), Amalone Pius (25), Frank Donatus (10), Alphonce Nyaland (26), Athanasia Reginald (14), Phillemon Ceressa (49), Neema Daud (13) Sophia Kanda (72), Theofrida Innocent (21), Regina Darnes (17).

Mesoit Siriri (33), Clenes Pius (22), Joyce Yohana (15), Restuta Alex (50), Mathias Riha (74), Magreth Andrew (45), James Gabriel (16), Regina James (17), Elizabeth Masawe (15), Elizabeth Sauli (18), Njau (35), Yasinta Msafiri (160) na Doreen Pancras (28).

Waliokuwa katika Hospitali ya St. Elizabeth kwa mujibu wa Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Dk Samwel Mlay ni Fatuma Tarimo, Glory Tesha, Rose Pius, Isabela Michael, Jenipher Joachim, Samwel Laswai, John James, Joan Temba, Joram Kisera, Novat John, Neema Kilusu, Regina Shirima, Inocent Charles, Lightness na Anna Edward.

Majeruhi wazungumza

 

Akizungumzia tukio hilo, Ndowe ambaye amelazwa Mount Metu, alisema aliona kitu kikidondoka kanisani na kutoa kishindo kikubwa na watu kuanza kukimbia ovyo. Alipoteza fahamu kutokana na kutokwa na damu nyingi.

Debora ambaye ni Polisi alisema alipoona kitu kikidondoka alibaini mara moja kuwa ni bomu. Alijeruhiwa mguu na mkono. Elizabeth alisema aliona kitu kama kibuyu kikianguka chini na kupasuka na baada ya hapo hakujua kilichoendelea.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magessa Mulongo alisema:

“Hili ni jambo la kusikitisha, kukera na kufadhaisha sana kutokea mkoani mwetu. Nawaomba wananchi wote tuwe watulivu wakati vyombo vya ulinzi na usalama vikiendelea na uchunguzi.”

Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema na Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari waliongoza mamia ya watu kutoa damu ili kuokoa maisha ya majeruhi.

Akizungumza kabla ya kutoa damu, Lema alisema msiba huo ni wa wakazi wote wa Arusha na akaomba usichochee mpasuko wa kidini kwani haijulikani nani waliohusika.

“Msiba huu ni wetu sote Wakristo na Waislamu, kikubwa ni kuomboleza na kulaani waliohusika na unyama huu na sote tuhakikishe tunasaidia kukamatwa kwa wote waliohusika,” alisema.

Bajeti ya Mambo ya Ndani leo

Tukio hilo limekuja siku moja kabla ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuwasilisha bungeni Dodoma leo, Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi yake kwa mwaka 2013/14.

Tukio hilo pamoja na matukio kadhaa yenye kuhatarisha umoja wa Watanzania yanayohusishwa na masuala ya dini yanatarajiwa kuchukua nafasi kubwa katika mjadala wa bajeti hiyo.

Imeandikwa na Mussa Juma, Moses Mashalla Peter Saramba na Daniel Sabuni.    

Watu 60 wahofiwa kufa Darfur

Uchimbaji wa madini ya dhahabu

Watu wapatao 60 wanahofiwa kufa baada ya mgodi wa dhahabu kuporomoka katika jimbo la Darfur nchini Sudan.

Waokoaji walikuwa wakitumia zana za asili kujaribu kuwafikia wachimbaji hao huku kukiwa na hofu kwamba visima zaidi huenda vikafunikwa.

Makundi hasimu Kaskazini mwa Darfur, yalikuwa yakipigana kugombea udhibiti wa mgodi huo mwazi Februari mwaka huu.

Dhahabu imekua bidhaa muhimu kwa Sudan tangu Sudan Kusini yenye utajiri mkubwa wa mafuta ijitenge miaka miwili iliyopita.

Kujitenga kwa Sudan Kusini kulisababisha Sudan kupoteza asilimia sabini na tano ya uzalishaji wa mafuta.

Serikali ya Sudan inatarajia kuzalisha takriban tani 50 za dhahabu mwaka 2013, ambayo huenda ikaifanya Sudan kuwa nchi ya tatu Barani Afrika kwa uchimbaji wa dhahabu na kuifikisha katika nafasi ya 15 ya wazalishaji wakubwa duniani.

Ukosefu wa vifaa vya uokozi

Uchimbaji wa madini ya dhahabu

Kwa mujibu wa afisa wa serikali, Haroun al Hassan kisima hicho chenye urefu wa mita 40, kwenye mgodi wa Jebel Amer Darfur Kaskazini kilifunikwa siku ya Jumatatu.

Kaimu Gavana wa Kaskazini Darfur, Al Fatieh Abdeaziz, ameiambia BBC kwamba watu 60 hawajulikani walipo, lakini hakuthibitisha kama wamekufa.

Bw. Hassan amesema juhudi za uokoaji zinakwamishwa na hofu kwamba visima zaidi huenda vikafunikwa. Amedai kuwa, waokoaji hawawezi kutumia mashine kwa sababu endapo zitafika karibu, ardhi itafunikwa.

Ameongeza kuwa, watu wanatumia zana za asili na kwa sababu hiyo, shughuli ya uokoaji inakwenda taratibu.

Umoja wa Mataifa umesema, watu wapatao 100,000 walikimbia mapigano baada ya makundi hasimu ya Kiarabu kupigana wakigombea udhibiti wa mgodi huo Februari mwaka huu.

Zaidi ya watu milioni moja wamekuwa wakiishi katika kambi za watu wasiokuwa na makazi Darfur, baada ya muongo mmoja wa mapigano.

Machafuko ya Darfur yamepungua baada ya kuzuka kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe mwaka 2003 lakini bado kuna mapigano kati ya vikosi vya serikali, waasi, wahalifu na makundi hasimu.

260,000 walikufa wakati wa ukame Somalia

Watoto wengi walikufa kutokana na utapia mlo

Takriban watu 260,000 walifariki dunia wakati wa ukame ulioikumba Somalia kuanzia mwaka 2010 hadi 2012, utafiti umebaini.

Nusu ya waliofariki dunia walikuwa ni watoto wenye umri chini ya miaka mitano, inaeleza ripoti ya shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo, FAO, pamoja Mtandao wa Kuonya Mapema Kuhusu Majanga ya Ukame unaofadhiliwa na Marekani.

Idadi ya vifo ilikuwa kubwa kuliko ile iliyokadiriwa ya watu 220,000 waliofariki wakati wa ukame wa mwaka 1992.

Janga hilo lilisababishwa na ukame mkali, uliochochewa na mapigano kati ya makundi hasimu yaliyokuwa yakigombea madaraka.

Umoja wa Mataifa kwa mara ya kwanza ulitangaza hali ya ukame Julai 2011 katika mikoa ya Somalia ya Bakool uliopo kusini na ule wa chini wa Shabelle, ambayo ilikuwa inadhibitiwa na kundi la wanamgambo wa Al – Shabab wenye mafungamano na Al – Qaeda.

Lakini kundi hilo lilikanusha kuwepo kwa hali hiyo na kuyapiga marufuku mashirika kadhaa ya misaada ya nchi za magharibi kufanya shughuli zake katika maeneo hayo.

Baadaye ukame ulisambaa katika maeneo mengine ukiwemo mkoa wa kati wa Shabelle na Afgoye na katika kambi za watu wasiokuwa na makaazi katika maeneo yaliyokuwa yakidibitiwa na serikali katika mji mkuu Mogadishu.

Mchumi Mwandamizi wa shirika la FAO, Mark Smulders amesema, ukweli kuhusu ukubwa wa janga hilo la kibinadamu umeibuka kwenye utafiti uliofanywa kwa kushirikiana na Mtandao wa Kuonya Mapema Majanga ya Ukame, Fews Net.

“Kwa kawaida, kukadiria vifo wakati wa dharura ni sayansi isiyo rasmi, lakini kutokana na ubora na kiwango cha takwimu zilizokuwepo, tuna uhakika na utafiti huo”, amesema ofisa wa Fews Net Chris Hillbruner.

“Utafiti huo unaeleza kuwa, kilichotokea Somalia ni moja ya majanga mabaya kabisa ya ukame kuwahi kushuhudiwa katika kipindi cha miaka 25 iliyopita, “ ameongeza.

Inakadiriwa kuwa 4.6% ya jumla ya idadi ya watu na 10% ya watoto chini ya umri wa miaka mitano walifariki dunia huko maeneo ya kusini na kati mwa Somalia, imeeleza ripoti hiyo.

“Ripoti hiyo imethibitisha kuwa hatua za ziada zingechukuliwa kabla ya ukame huo haujatangazwa, amesema Phillippe Lazzarini, Mratibu wa Shughuli za Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia.

Somalia ilikumbwa na ukame mkali mwaka 2011, ulioathiri zaidi ya watu milioni 13 katika eneo lote la Pembe ya Afrika.

Maelfu ya watu walikimbia makaazi yao wakisaka chakula. Umoja wa mataifa ulitangaza ukame huo kumalizika Februari 2012.

Kwa zaidi ya miaka 20 ya vita vya weyewe kwa wenyewe, Somalia imeshuhudia wababe wa kivita wa koo, wanasiasa mahasimu na vikundi vya wanamgambo vikigombea madaraka, hali iliyoruhusu kushamiri kwa ukosefu wa utawala wa sheria.

Septemba mwaka jana, serikali inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa iliingia madarakani baada ya miaka nane ya utawala wa mpito, hatua iliyoleta utengamano katika baadhi ya maeneo.

JICHO LETU KATIKA MAGAZETI MAY 3

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.

Mwanajeshi wa Ufaransa auawa Mali

Ufaransa inatarajiwa kuanza kuwaondoa wanajeshi wake nchini Mali

Mwanajeshi mmoja wa Ufaransa nchini Mali ameuawa na wengine wawili kujeruhiwa vibaya.

Kwa mujibu wa maafisa wa Ufaransa, mwanajeshi huyo kutoka kikosi maalum cha Ufaransa aliuawa Magharibi mwa nchi baada ya gari lake kulipukiwa na bomu lililokuwa limetegwa kando ya barabara.

Hadi kufikia sasa wanajeshi sita wa Ufaransa wameuawa tangu Ufaransa kuanza operesheni yake dhidi ya wapiganaji wa kiisilamu waliokuwa wanadhibiti Kaskazini mwa nchi

Ufaransa ilitangaza kuanza kuondoa baadhi ya wanajeshi wake 4,000 walioko Mali.

Lakini wengine 1,000 watasalia nchini humo hadi mwakani kuweza kukabiliana na wapiganaji wa kiisilamu walio na uhusiano na kundi la Al-Qaeda

Baadhi ya miji, imeweza kudhibitiwa na wanajeshi hao, lakini wapiganaji hao wangali kwenye maficho yao ya mwisho Kaskazini mwa Mali ambako wanafanya mashambulizi ya kuvizia dhidi ya wanajeshi wa Mali na Ufaransa.

Hivi maajuzi Umoja wa Mataifa uliafikia kunda kikosi cha wanajeshi 12,000 kushika doria nchini Mali.

Watashirikiana na kikosi cha wanajeshi 6000 ambao tayari wako nchini humo.

Rais Francois Hollande ametoa rambi rambi zake kwa familia za waliouawa huku akiwasifu kwa ujasiri wao nchini Mali.

Mbunge: Sikukimbia mafunzo JKT



Mbunge wa Jimbo la Tarime (CCM), Nyambari Nyangwine ameibuka na kukanusha taarifa kwamba alikimbia mafunzo maalum ya wiki tatu ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) yaliyowashirikisha wabunge 47.

Mbunge huyo awali alipangiwa kambi ya Mlale iliyopo Songea, kabla ya kubadilisha na kuhamishiwa kambi ya JKT Ruvu, alitoweka ikiwa imebaki wiki moja ahitimu mafunzo hayo yaliyofanyika katika vikosi mbalimbali nchini, wabunge 23 tu ndio waliofanikiwa kuhitimu.

Mafunzo hayo ya awali kwa wabunge yalifungwa na Rais Jakaya Kikwete Machi 26 mwaka huu, ambapo pia alizindua mafunzo ya miezi mitatu ya Jeshi hilo kwa vijana 4,710 nchi nzima kwa mujibu wa sheria.

Baadhi ya waliohitimu mafunzo hayo Ester Bulaya, Halima Mdee, Neema Hamid, David Silinde, Murtaza Mangungu, Livingston Lusinde, Yusuph Khamis, Said Mtanda na Mendrad Kigola.

Akizungumza Dar es Salaam jana,Nyangwine alisema alishiriki mafunzo mbalimbali, lakini ilipofikia wakati wa kufanya mafunzo msituni aliugua.

“Sikwenda katika zoezi la msituni kwa sababu daktari alinipima na kugundua kuwa nilikuwa na tatizo la shinikizo la damu(BP), kutokana na presha yangu kupanda bila sababu za msingi nilitakiwa kupumzika” alisema Nyangwine.

Alisema licha ya kupumzika bado hali yake ilikuwa mbaya, hivyo kulazimika kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), ambapo alitakiwa kupumizia kwa zaidi ya siku mbili.

“Kule kambini walinipa ruhusa ambayo haikueleza siku ambayo natakiwa kurudi. Baada ya kupata nafuu wenzangu walikuwa wameshamaliza, lakini cheti changu cha JKT kipo na muda wowote naweza kwenda kukichukua” alisema

Alisema alishindwa kuhudhuria sherehe za kutunukiwa vyeti kwa kuwa alikwenda Mwanza kushiriki mkutano wa wabunge ambao majimbo yao yamezungukwa na hifadhi za wanyamapori.

Mafunzo ya JKT yalianza tena baada ya kufutwa kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita kutokana na kuyumba kwa uchumi, lakini kutokana na umuhimu, Serikali sasa imeamua kuyarudisha ingawa bado yanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na fedha.

Tuhuma nzito: Chadema yamtuhumu Kinana kuhusika na biashara ya pembe za ndovu

Abdulrahman Kinana 

Dodoma. Kambi ya Upinzani Bungeni imetoa tuhuma nzito kwa Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana ikidai kuwa anajihusisha na mtandao wa ujangili nchini.
Hata hivyo, Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi amejibu tuhuma hiyo akisema ni za uongo huku akiituhumu kambi hiyo kuwa imedanganya wakati inajua ukweli kuhusu tuhuma dhidi ya Kinana.
Akiwasilisha maoni ya upinzani kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii mwaka 2013/14, Msemaji wa Kambi ya Upinzani kuhusu Maliasili, Mchungaji Peter Msigwa alisema vitendo vya ujangili vimekuwa vikilitia doa taifa kwenye jumuiya za kimataifa.
“Kwa bahati mbaya ni kwamba wahusika wengi ambao wanatajwa kwa ushahidi ni makada maarufu na wengine ni viongozi waandamizi wa CCM,” alisema Mchungaji Msigwa.
“Tumeshuhudia watuhumiwa wengine wa ujangili ambao Ikulu imediriki kuwapatia nafasi kubwa za uongozi wa taifa hili, licha ya kutajwa kwenye ripoti ya uchunguzi kuhusiana na ujangili.”
Alisema mwaka 2009, meli ya Kampuni ya Wakala wa Meli ya Sharaf Shipping inayomilikiwa na Kinana ilikamatwa China ikiwa na makontena yenye nyara za Serikali ikiyasafirisha kwenda Hong Kong.
“Nyaraka zilizopo Ofisi za Wakala wa Usajili wa Kampuni na Biashara (Brela), zinaonyesha kuwa kampuni hiyo ya Kinana ilisajiliwa Oktoba 2003 na kupewa hati na. 47221.
“Nyaraka zinaonyesha kuwa Kinana anamiliki hisa 7,500 kati ya 10,000 za kampuni hiyo iliyosajiliwa Dar es Salaam. Mshirika mwenzake katika kampuni hiyo, Rahma Hussein ambaye ni mke wake anamiliki hisa 2,500,” alisema Msigwa.

Dk Nchimbi ajibu mapigo
Akijibu tuhuma hizo, Waziri Nchimbi alisema: “Ukiona mtu anasimama na kuamua kusema kuwa hakuna kinachofanywa na wizara kuhusu masuala ya ujangili, ni wazi uelewa wake unakuwa na utata mkubwa.”
Alisema hoja zilizojengwa dhidi ya Kinana ni uongo mtupu... “Nimejaribu kufuatilia kwa makini alichokisema alikimaanisha, alikielewa, alikitafakari au aliandikiwa tu akaenda kusoma? Baada ya kutafakari kwa kina nikagundua hakuwa na nia mbaya, aliandikiwa tu na ameenda kusoma,” alisema Dk Nchimbi.
Alisema ukweli wa jambo hilo ni kwamba ipo tofauti ya majukumu ya kampuni za Wakala wa Meli na shughuli za kupakia mizigo bandarini huku akituhumu kambi ya upinzani kuwa inajua ukweli lakini imeamua kupotosha umma.
Dk Nchimbi ambaye alikuwa mchangiaji wa kwanza, alisema wakala hawezi kuwa mmiliki wa meli, bali anamwakilisha mwenye meli kwenye shughuli ndogondogo zinazofanyika inapofika nchi fulani kama kuhudumia watumishi wa meli, mahitaji muhimu na kufanya usafi.
“Lakini kuna watu wanaitwa ‘clearing and forwarding (Kupakua na kupeleka mizigo). Napenda kukwambia Mchungaji Msigwa kuwa kazi yao ni kupeleka na kutoa mizigo bandarini,” alisema Dk Nchimbi na kuongeza;
“Kule ndiko kuna utaratibu wa upekuzi, katika utaratibu wa upekuzi mtu wa ‘shipping agency’ (wakala wa meli) hahusiki, sina shaka hata kidogo Mchungaji Msigwa analijua hili ninalolisema, ila amelifumbia macho kwa makusudi kwa masilahi yasiyokubalika katika taifa.”
Alisema kumekuwa na uvumi ambao umekuwa ukifanywa kwa makusudi kuwa Kinana anahusika na meli iliyohusika kusafirisha pembe zile.
“Uvumi huu ni uzushi, meli iliyobeba mizigo ile inaitwa Delmas Nakadha, mmiliki wake anaitwa Bus Herman Ledley jambo hili Kambi ya Upinzani Bungeni inalijua, ila kwa masilahi yasiyokubalika katika taifa wameamua kupotosha Bunge lako,” alisema.
Alisema baada ya uchunguzi wa kutosha, wahusika walibainika na ikafunguliwa kesi ya uhujumu uchumi namba 3 na 4 ya mwaka 2009 kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.
“Hawa (anawataja) ndiyo waliopelekwa kortini, uchunguzi ulijidhihirisha kuwa ndiyo watuhumiwa wa jambo hili, Kambi ya Upinzani Bungeni inalijua,” alisema.

JICHO LETU KATIKA MAGAZETI MAY 1

.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.
.